Kiongozi wa kanisa Katoliki duniani Papa Francis amekutana na kansela wa Ujerumani anayemaliza muda wake Angela Merkel. 

Merkel amechagua Vatican na Rome kuwa vituo vyake vya mwanzo vya ziara yake ya kuagana na viongozi duniani baada ya miaka 16 ya Ukansela. 

Hii ni mara ya saba kwa Papa kukutana na Merkel na kumfanya mwanamama huyo kuwa kiongozi aliyekutana mara nyingi zaidi na kiongozi huyo wa kanisa Katoliki ulimwenguni. 

Baada ya mkutano na papa, Merkel alikutana na waziri mkuu wa Italia Mario Draghi na mchana wa leo alihudhuria sala ya kuombea amani akiwa na Papa Francis na askofu wa jimbo la Canterbury Justin Welby. 

Kwenye ziara hiyo kansela Merkel amemtolea mwito Papa kukabiliana na vitendo vya unyanyasaji dhidi ya watoto vinavyofanywa na kanisa hilo.