Hukumu ya kesi ya unyang’anyi wa kutumia silaha inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya na wenzake wawili iliyokuwa itolewe leo imeahirishwa hadi Oktoba 15, 2021.

Akiahirisha hukumu hiyo Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, Amalia Mushi amesema bado hukumu hiyo haijakamilika kuandikwa.

Sabaya na wenzake, Sylvester Nyegu na Daniel Mbura, wanakabiliwa na mashtaka matatu ya unyang’anyi wa kutumia silaha. Inadaiwa katika shtaka la kwanza kuwa Februari 9, 2021 katika Mtaa wa Bondeni, Arusha, washtakiwa hao waliiba Sh2.769 milioni, mali ya mfanyabiashara Mohamed Saad.

Upande wa mashtaka ulidai kuwa kabla na baada ya kufanya wizi huo, washtakiwa waliwashambulia Numan Jasin, Harijin Saad Harijin, Bakari Msangi, Salim Hassan na Ally Shaban kwa kuwapiga kwa kutumia bunduki, ili kufanikisha wizi huo.