Mahakama  ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Arusha, leo inatarajia kutoa hukumu katika kesi ya jinai namba 105 ya unyang’anyi wa kutumia silaha inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, mkoani Kilimanjaro, Lengai Ole Sabaya (34).

Washtakiwa wengine katika shauri hilo ni Silvester Nyegu(26) na Daniel Mbura(38), ambao wanakabiliwa na mashtaka matatu ya unyang'anyi kwa kutumia silaha.

Kesi hiyo ilinguruma kwa siku 35 mfululizo mbele ya Hakimu Mwandamizi wa mahakama hiyo, Odira Amworo hadi kufikia tamati.

Upande wa Jamhuri ulikuwa na mashahidi 11 na vielelezo 10 vya ushahidi na viliwasilishwa mahakamani kama sehemu ya ushahidi.

Mashahidi wa upande wa utetezi, walikuwa watatu na walijitetea kwa njia ya kula kiapo na kuwasilisha baadhi ya nyaraka kama vilelezo vya ushahidi.