Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango amesema bado kasi ya ukuaji wa sekta ya viwanda nchini ni mdogo na hivyo kuitaka Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kushirikiana na Shirikisho la Viwanda (CTI) kufanya tafakuri ya kina kupata suluhu ya changamoto zinazokwamisha Sekta hiyo.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati wa hafla ya utoaji wa Tuzo za Rais kwa wazalishaji bora wa viwandani nchini, hafla iliofanyika katika hoteli ya Serena Jijini Dar es salaam.

Amesema bado bidhaa zinazozalishwa hapa nchini hazijakidhi mahitaji ya wananchi na baadhi kutokidhi viwango vya soko hivyo kuendelea kuagiza bidhaa za viwandani kutoka nje ya nchi. Makamu wa Rais ametaja baadhi ya bidhaa zilizotumia gharama kubwa kwa kuagizwa kutoka nje ya nchi mwaka 2020 kama vile shilingi bilioni 200 kutumika kuagiza bidhaa za vitambaa ikiwa pamba inazalishwa hapa nchini.

Aidha Makamu wa Rais amesema ni muhimu wa Shirikisho la Viwanda nchini kwa kushirikiana na serikali kutumia Balozi za Tanzania katika maeneo mbalimbali duniani kutafuta masoko zaidi ya bidhaa zinazozalishwa hapa nchini.

Makamu wa Rais ametoa rai kwa watanzania kutumia bidhaa zinazolishwa hapa nchini ili kuendelea kukuza viwanda vya ndani ya nchi pamoja kutengeneza ajira zaidi kwa watanzania.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Shirikisho la Viwanda nchini (CTI) Paul Makanza ameishukuru serikali ya awamu ya sita kwa kutatua kwa haraka changamoto zilizokuwa zinaikabili sekta ya viwanda nchini ikiwemo namna ya ukusanyaji wa kodi pamoja na upatikanaji wa vibali vya kazi kwa wataalam kutoka nje ya nchi


Awali akimkaribisha Makamu wa Rais, Waziri wa Viwanda na Biashara Prof Kitila Mkumbo amesema kwa kutambua umuhimu wa sekta ya nishati hapa nchini kwa maendeleo ya viwanda, serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuboresha sekta hiyo ikiwa ni pamoja na kuondoa tozo mbalimbali ili kuhakikisha bei ya mafuta haipandi kwa kiasi kikubwa nchini licha ya kupanda katika soko la dunia.