Na. John Mapepele, WUSM
Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe, Innocent Bashungwa ameomba mashindano ya Kombe la Taifa, (Taifa CUP) yaliyorejeshwa na Wizara yake mwaka huu kuitwa Kombe la Taifa la Mama Samia (Samia Taifa CUP) kutokana na uzito wa mashindano hayo na nia njema ya Mhe, Rais ya kuendelea michezo nchini.

Mhe. Bashungwa ameyasema hayo  Oktoba 27, 2021 kwenye hafla ya kupongeza timu ya soka ya Taifa ya Wanawake (Taifa Stars) iliyoandaliwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mhe, Samia Suluhu Hassan jijini Dar es Salaam alipokuwa akifafanua  mafanikio ya Sekta za Utamaduni, Sanaa na Michezo katika kipindi hiki.

Akielezea mafanikio hayo amesema kuwa ni pamoja na kuandaa mkakati pamoja  baina ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Baraza la Michezo la Majeshi Tanzania (BAMMATA) na Baraza la Michezo la Taifa (BMT) kwenye mashindano ya kimataifa na kuongeza kuwa wachezaji  46 wanacheza michezo ya kulipwa nje ya nchi.

Kuhusu maelekezo ya Mhe. Rais ya kuwa na shule za michezo nchini, Mhe. Bashungwa amesema  hadi sasa  zimeshatengwa shule za michezo 56 ambapo ni mbili kila Mkoa ambazo zitakuwa zinatoa masomo maalum ya michezo  na  kwamba shule hizo zitapatiwa  vifaa na walimu kwa ajili ya michezo.

Amesema  tayari shilingi  bilioni 1.6 zimetengwa kwa ajili ya  chuo cha michezo (National Sports Academy) cha Malya mkoani Mwanza pia michoro kwa ajili ya kumbi za kisasa za michezo (sports Arena) zinatarajiwa kukamilika  mwezi ujao.

Aidha, amesema Wizara imeandaa mpango mkakati ambao umeainisha michezo  michache (6) ya kipaumbele ili iweze kufanya vizuri na kufika kwenye ngazi  ya kimataifa.

Pia, katika kuendeleza michezo kwa wanawake Tamasha la michezo la Wanawake la Tanzanite lilifanyika Septemba 16-18, 2021 jijini Dar es Saaam ambapo litaendelea kuboreshwa na kuwepo kila mwaka ili kuibua vipaji vya wanawake.

Amesema hadi sasa tayari Wizara imekamilisha marekebisho ya uwanja wa Taifa wa ndani ambao umetoa fursa ya kufanyika kwa mashindano ya Kanda ya Afrika ya Kikapu kwa wanaume na wanawake yanayoanza Oktoba 29,2021 ambapo zaidi ya nchi kumi zinashiriki.

Pia maboresho ya uwanja wa Mkapa na uhuru yamekamilika yanayotoa fursa ya kufanyika kwa mashindano ya Afrika ya Soka kwa walemavu Novemba  mwaka huu, na kuongeza kuwa michezo ya SHIMIWI imerejeshwa ambayo ilifunguliwa  Oktoba 23,2021 na Makamu wa Rais.

Bashungwa amefafanua kuwa endapo Wizara itawezeshwa zaidi, na mikakati iliyojiwekea pamoja na maelekezo yanayotolewa na viongozi wakuu  michezo, Sanaa na utamaduni utafiuka mbali.

Akitambulisha wageni wa Wizara kwenye tukio hilo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Hassan Abbasi amemshukuru Mhe. Rais kwa kuleta mapinduzi makubwa kwenye Sekta za Utamaduni, Sanaa na Michezo na kumwahidi  kuendelelea kusimami  kikamilifu ili kuendeleza michezo.