Na. Edward Kondela
Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki ameagiza maafisa mifugo na madaktari wa mifugo, Wilaya ya Bariadi Mkoani Simiyu, walioandika au kushuhudia vyeti vya vifo vya ng’ombe zaidi ya 270 ambao walikamatwa na uongozi wa Pori la Hifadhi la Maswa kusakwa na kufikishwa katika Baraza la Veterinari Tanzania ili kuchunguzwa.

Waziri Ndaki amebainisha hayo (16.09.2021) wakati alipofanya ziara ya kikazi ya siku moja katika Wilaya za Itilima na Meatu ambapo akiwa katika Wilaya ya Itilima aliarifiwa baadhi ya wafugaji walioshinda kesi Mahakama ya Rufaa mwaka 2019, baada ya ng’ombe wao kudaiwa kuingia katika Pori la Hifadhi la Maswa mwaka 2017, kurejeshewa ng’ombe 51 pekee huku uongozi wa pori hilo ukiwaarifu ng’ombe zaidi ya 270 walikufa, bila wafugaji hao kushuhudia mizoga ya ng’ombe hao wala vyeti vya vifo ambavyo inaelezwa viliandikwa na maafisa mifugo ambao pia hawakushudia mizoga hiyo.

Ameongeza kuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa sasa inafuatilia taarifa za wafugaji kote nchini, ambao mifugo yao ilikamatwa na baadaye wafugaji hao kushinda kesi lakini mifugo hiyo haijareshwa kwao wala fedha walizolipishwa faini, kufuatia agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan kutaka taarifa hiyo ambayo wizara inakusanya ili kuifikisha kwa Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa kwa ajili ya maamuzi zaidi.

“Maafisa mifugo na madaktari wa mifugo nchi nzima mnapaswa kujua nyie ni madaktari wa mifugo siyo kukaa kwenye meza na kuandika vyeti vya vifo vya ng’ombe bila kushuhudia vifo hivyo, baadhi yenu wanafanya kazi kiholela.” Amesema Mhe. Ndaki

“Hili jambo siyo dogo ni kubwa nimeagizwa na Rais nije kufuatilia masuala haya watu wameshinda kesi lakini ng’ombe hawajarudishwa kwa wenyewe, nimeambiwa nifuatilie nipeleke orodha yote kwa waziri mkuu ili taarifa itolewe.” Amefafanua Mhe. Ndaki

Kuhusiana na ng’ombe zaidi ya 270 ambao hawajulikani walipo Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amemjulisha afisa mifugo Mkoa wa Simiyu kwamba wizara inataka kujua aliyeandika vyeti vya vifo vya ng’ombe hao ambavyo havijulikani vilipo na wala ushahidi wa kuwa ng’ombe hao walikufa, huku akionya maafisa mifugo na madaktari watakaobainika kuendelea kufanya kazi bila kufuata taratibu za kazi zao Baraza la Veterinari Tanzania halitasita kufuta usajili wao.

Aidha, Waziri Ndaki amewaelekeza wakuu wa Wilaya za Itilima na Meatu kufikia Siku ya Jumanne (21.09.2021) wawe wamefikisha taarifa rasmi wizarani juu ya idadi ya mifugo iliyokuwa imekamatwa na kurejeshwa kwa wafugaji, idadi ambayo haijarudishwa pamoja na majina ya wafugaji ambao wanadai mifugo yao baada ya kushinda kesi mahakamani kwa madai kuwa mifugo yao iliingia katika Pori la Hifadhi la Maswa.

Katika nyakati tofauti akiwa katika Wilaya za Itilima na Meatu baadhi ya wafugaji wamelalamikia kitendo cha baadhi ya maafisa wa serikali, kutoheshimu maamuzi ya mahakama ambapo ndiyo chombo cha mwisho katika kutoa haki kwani maamuzi yametolewa siku nyingi lakini baadhi ya wafugaji hawajui hatma ya mifugo yao iliyokamatwa hali iliyosababisha kuwa na maisha duni.

Pia wamemuomba Waziri Ndaki kuwa, serikali iangalie namna ya kuwaruhusu wafugaji kuvuna malisho katika maeneo ya hifadhi badala ya malisho hayo kuchomwa moto ili wafugaji wawe wanayavuna na kuyatunza kwa ajili ya mifugo yao.

Wamebainisha kuwa wamekuwa wakipata shida ya malisho kutokana na baadhi ya maeneo kuwa na ukame, hali ambayo inawapa wakati mgumu kwa mifugo yao kuwa na malisho ya uhakika.

Katika hatua nyingine, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mashimba Ndaki amewahimiza wafugaji kuiwekea mifugo yao hereni za kieletroniki ambazo zinatambua mfugo ulipo kuanzia ngazi ya taifa hadi kijiji hali ambayo itasaidia kuzuia wizi na upotevu wa mifugo.

Mwisho.