Kaimu meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Arusha, Kayobyo Majogolo(41) ambaye ni  shahidi wa pili katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili  aliyekuwa mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya na wenzake sita  ameieleza mahakama kuwa kwa mujibu wa sheria anayepaswa kukusanya kodi ni mamlaka hiyo tu.

Akiongozwa kutoa ushahidi wake na wakili wa Serikali mwandamizi, Ofmed Mtenga mbele ya hakimu mkazi, Patrisia Kisinda shahidi huyo amedai kuwa kwa mujibu wa sheria mwenye mamlaka ya kuunda kikosi kazi maalum ni kamishna mkuu wa TRA.

Ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha kuwa mkuu wa wilaya hawezi kuwa na jukumu la kukusanya kodi.

Katika shauri hilo la uhujumu namba 27,2021, washtakiwa wengine ni Enock Mnkeni, Watson Mwahomange, John Aweyo, Sylvester Nyegu, Jackson Macha na Nathan Msuya.