SERIKALI ya Tanzania imeahidi kulisaidia Kundi la Vijana linakuwa katika Mazingira bora na endelevu kupitia Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana inayoandaliwa kupitia Rasimu ya Sera hiyo inayoshirikisha na inayopendekezwa na vijana hao wa kada mbalimbali.

Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa idara ya Maendeleo ya Vijana Mkuu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Julius Tweneshe katika Kikao cha kujadili Rasimu ya Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana kilichofanyika Dar es Salaam kilichowakutanisha vijana wa mikoa ya Dar, Lindi, Mtwara, Pwani na Tanga.

Tweneshe amesema lengo kuu la kukutana na Vijana hao ilikuwa kujadili masuala mbalimbali sambamba na taifa zima yakiwemo masuala ya Uchumi, Afya, Uwezeshwaji Kiuchumi, Ubunifu, masuala ya Diplomasia, Mazingira wezeshi katika Biashara, Kilimo, Upatikanaji wa Ajira na mengineyo.

“Kuna Kamati maalum imeundwa kwa kupitia maoni ya Vijana na baadae kupata taratibu ili kuboresha Sera kwa Vijana wa Taifa lote la Tanzania. Maoni yao watayatoa kwa njia ya kuzungumza na kuwasilisha kupitia Fomu maalum iliyoandaliwa”, amesema Tweneshe.

Kwa upande wao Vijana wameomba Rasimu hiyo kufanyiwa kazi ipasavyo kwa maoni yao mazuri kuchukuliwa ili kupata Sera bora ya Maendeleo ya Taifa kwa Vijana. “Serikali kupitia Rasimu hii inapaswa kuangalia changamoto za Vijana ili kuzitatua sambamba na kuwasaidia vijana kufika malengo yao”, amesema mmoja wa Vijana, Paul Makoye.

Naye Kijana Tatu Kassim Sultan, mwenye ulemavu wa Ngozi amependekeza kuwa Vijana wa makundi maalum wapewe kipaumbele katika masuala mbalimbali yakiwemo masuala ya Ajira ili kuondokana na vitendo vinavyoashiria unyanyapaa kwa jamii inayowazunguka.

Hii ni mara ya tatu kwa mapitio ya Rasimu ya Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana yanafanywa kwa mwaka huu wa 2021 baada ya kwanza kufanyika mwaka 1996 na 2007. Kundi linahusishwa zaidi kujadili Rasimu hiyo ni Asasi za Maendeleo za Kiraia, Wawakilishi wa Vijana kutoka Makundi maalum, Wawakilishi wa Vyama vya Siasa na makundi mengine.