Serikali ipo katika mchakato wa kufanya mapitio ya sheria na kanuni zinazo simamia sekta ya uvuvi nchini ili kukuza na kuendeleza viumbe maji ikiwemo ufugaji samaki kwa kutumia vizimba.

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki amebainisha hayo leo Septemba 24,2021 jijini Dodoma wakati alipozungumza na waandishi wa habari mara baada ya kushiriki mkutano wa kimataifa wa kukuza na kuendeleza ukuzaji viumbe maji ulifanyika kwa njia ya video.

Mashimba, amesema lengo la kupitia sheria pamoja na kanuni katika sekta hiyo ni kuhakikisha kuwa zinawezesha uvuvi wa kutumia vizimba pamoja na mabwawa.

“Sheria pamoja na kanuni zetu awali sekta hii ya uvuvi ilikuwa imemezwa na uvuvi wa majini tuu hivyo tunafanya mapitio ili kuwezesha uvuvi huu wa kutumia vizimba unakuwa na mchango katika kuongeza pato la taifa”amesema Mashimba

Akizungumzi mkutano huo amesema lengo lake ni kuwezesha nchi washiriki kukuza na kuendelea ukuzaji wa viumbe maji kwa kutumia uvuvi wa vizimba, mabwawa pamoja na njia nyingene zisikuwa za bahari au ziwa.

“Pia katika mkutano huu tunaangalia changamoto pamoja na fursa zilizopo, vipaumbele na namna ya kuendeleza uvuvi wa viumbe maji”amesema Ndaki

Amesema uvuvi huo unamchango mkubwa katika usalama wa chakula ambapo hivi sasa sekta hiyo inachangia pato la taifa kwa asilimia 1.7.

“Kwenye samaki tunapata protini kwa asilimia 21 na takwimu zinaonyesha kuwa kuna kipindi tulipanda hadi kufikia mtu mmoja kula kilo 14, kwa mwaka lakini mwaka 2020, tumeshuka hadi mtu mmoja kula kilo 8.5 kwa mwaka”amesema

Kutokana na hali hiyo amesema Taifa linatakiwa kuwa na uvuvi endelewvu unaochangia usalama wa chakula na kukabilina na mabadiliko tabianchi.

“Tumekubalina kuwa na ushirikiano wetu wa namna ya kupeana utaalamu wa kukabiliana na mabadiliko tabianchi ili kuwa na uvuvi endelevu utakao kuza pato letu lakini pia pato la dunia kupitia sekta hii”amesisitiza

Vilevie, amesema mkakati wa serikali ni kuhakikisha inafanya utafiti wa maeneo kwa ajili ya ufugaji samaki kwa njia ya vizimba.

“Ili kuwasaidia watu wanaohitaji kufuga samaki kwa njia hii serikali inafanya utafiti wa mazingira kwa ajili ya ufugaji ili kuwaondolea gharama wananchi watakao hitaji kwakuwa gharama zake ni kubwa”amesema

Kadhalika, amesema mkakati mwingine ni kuhakikisha kuwa vituo vitano vya ukuzaji viumbe maji vinaboresha na kuzalisha vifaranga vya samaki kwa wingi na vyenye ubora.

“Lakini pia serikali inampango wa kuanzisha mashamba darasa kila wilaya kwa ajili ya kufundisha wakulima pamoja na wafugaji ufugaji wa samaki kwa kutumia vizimba na mabwawa”amesema