Rais Samia Suluhu Hassan jana amezindua Mkakati wa Uelimishaji na Uhamasishaji wa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 katika uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma.

Rais amesema sensa ina lengo la kufahamu idadi ya watu, mahali walipo, jinsia, rika, elimu, ajira, shughuli, makazi yao, mahali yalipo na hali yake.

Amesema taarifa hizo zitasaidia kufahamu wastani wa ongezeko la idadi ya watu katika nchi na pia hali ya uhamiaji kutoka vijijini kwenda mijini na kuwezesha nchi kutambua hatua mbalimbali za kimaendeleo.

Aidha, sensa inasaidia serikali kufanya maamuzi kuhusu ugawaji wa rasilimali za Taifa na kupeleka huduma mbalimbali za jamii kwa wananchi ikiwa ni pamoja na ujenzi wa miundombinu kwenye maeneo yao kulingana na idadi ya watu na mahitaji.

Aidha, itawezesha kutambua idadi ya majengo na mahali yalipo, itawezesha kufahamu hali ya mahitaji ya makazi nchini na kufahamu na kupanga mitaa kupitia anuani za makazi ambazo zitachochea benki kutoa mikopo na kupunguza viwango vya riba.

Rais ametoa wito kwa viongozi wa serikali, dini na vyama vya siasa kusisitiza wananchi kushiriki kikamilifu kwenye zoezi hilo la sensa.