Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limeandaa warsha ya kukuza uelewa wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira na Kanuni zake ikiwemo udhibiti wa Kelele na Mitetemo kwa viongozi wa Dini iliyofanyika katika Ukumbi wa Kisenga- Milenium Towers Makumbusho jijini Dar es Salaam.

Warsha hiyo imehudhuriwa  na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Amos Makalla, Mwenyekiti  wa Bodi ya Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC)Mhandisi Prof. Esnat Chaggu na Mkurugenzi Mkuu wa (NEMC)  Mhandisi Dkt. Samuel Gwamaka pamoja na Viongozi wa dini.

Akifungua Warsha hiyo , Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Amos Makalla amesema kuwa suala la kutoa elimu ni jambo la msingi kwani inasaidia kukuza uelewa kwa kila mtu. Amesema kuwa amepokea malalamiko mengi kutoka kwa Wananchi wa Mkoa wa Dar es Salaam kutokana na kelele na mitetemo.  

“Hivi karibuni nimefanya ziara ya kusikiliza kero za Wananchi  Mkoa wa Dar es Salaam kero ambazo nimezipokea takribani kero mia tisa ishirini na saba (927) zinahusu ardhi, miundombinu, Mirathi na kelele. Kelele zinazolalamikiwa ni kutoka Baa, kumbi za starehe pamoja na nyumba za ibada, hivyo nilipoalikwa katika warsha hii japo nina majukumu mengi lakini niliona bora nije hapa  maana nimeona  ndio nafasi pekee ambayo nitapata fursa kuzungumza nanyi”.  Amesema Mhe. Makalla

Aidha ameeleza kuwa  tafiti zilizofanyika katika kipindi cha hivi karibuni imebainika kuwa  malalamiko  ya uchafuzi wa kelele ni asilimia 85 ambayo 65 kutoka kumbi za starehe na 20 kutoka nyumba za ibada. Hivyo kutokana na tafiti hiyo Mhe. Makalla anaamini kuwa  semina hii itakuwa chachu ya kutafakari  na kuona kama Makanisa na Misikiti yapo sehemu sahihi ya kufanya ibada. Ameendelea kusema kuwa  kelele zina athari nyingi sana ikiwemo kukosa usikivu, umakini na usingizi kwa yule ambaye anasikiliza kelele hizo.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya NEMC Prof. Muhandisi Esnat Chaggu amesema kuwa Baraza kuandaa Warsha hii kwa kuwaita viongozi wa Dini na kutoa elimu kwao juu ya Sheria ya Mazingira na Kanuni yake ikiwemo kelele na mitetemo basi imeheshimu sana uwepo wa Mungu, hivyo basi  tunaamini kuwa suala hili limeisha na haliwezi kuwa tatizo kwa jamii yetu

Kwa Upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Dkt. Samuel Gwamaka ametoa shukrani kwa muitikio mkubwa kutoka kwa viongozi wa Dini katika warsha hiyo na amesema kuwa  NEMC imeona umuhimu wa kutoa elimu kwa jamii juu ya Sheria ya Mazingira na Kanuni zake ikiwemo kelele na mitetemo.

“tumeitisha semina hii kwa ajili ya kukuza uelewa wa athari za kiafya na kijamii kutokana na kelele na mitetemo. NEMC tumekuwa tukipokea malalamiko mengi kutoka kwa Wananchi juu ya kelele na mitetemo kutoka Baa, Kumbi za Starehe na Nyumba za Ibada hivyo tumeona ni bora tutoe elimu ili kuweza kuzingatia Sheria ya Mazingira na Kanuni  zake ili kuepusha uchafuzi wa kelele pamoja na malalamiko kutoka kwa wananchi.” Amesema Dkt. Gwamaka  
 
Mhe. Makalla amemaliza kwa kusema kuwa mwisho wa semina hii itasaidia kila mtu kuwa  kiongozi kwa mwengine juu ya kuzuia kelele kwa mujibu wa sheria na Kanuni zake. Pia amesema kuwa  jambo lingine la kutafakari ni katika mamlaka  za serikali hasa Wizara ya Ardhi na Mipango miji kufanya kazi kwa karibu sana na Taasisi za Dini ili tuweze kusaidia jamii ni kujua sehemu ipi sahihi kwa shule, makazi,uwanja wa mikutano wa wananchi, maeneo ya kuzikia pamoja na sehemu ya nyumba za ibada. Kama tutazingatia hilo basi malalamiko na kero kwa wananchi hazitakuwepo tena.