Na Munir Shemweta, DODOMA
Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula amesitisha zoezi la uzinduzi uuazaji nyumba 300 za mradi wa Uyumbu iliopo katika jiji la Dodoma mpaka hapo Shirika la Nyumba la Taifa litakapokamilisha ujenzi wa mradi huo.

Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) hivi karibuni limetangaza kuanza uzinduzi rasmi wa uuzaji nyumba 300 kwenye mradi wake wa nyumba 300 katika eneo la Iyumbu siku ya jumanne tarehe 14 Septemba .

Akizungumza alipofanya ziara ya kushtukiza kwenye mradi huo leo tarehe 10 Septemba 2020 jijini Dodoma, Dkt Mabula alisema lengo la wizara ya Ardhi ni kuwa, mradi wa nyumba hizo ukamilike ndipo nyumba hizo zianze kuuzwa kwa wale wananchi wanaozihitaji.

‘’Makubaliano kazi za ujenzi wa nyumba zinakwisha kwanza na mtu anapewa funguo na hati yake lakini leo utapomuuzia mtu nyumba ambayo haijakamilika unamuuzia nini ? au unamuuzia nyumba in progress, lengo letu ni kumuuzia nyumba iliyokamilika’’ alisema Dkt Mabula.

Hata hivyo, Naibu Waziri aliongeza kuwa, wale wananchi wanaohitaji kununua nyumba hizo wanaweza kuonesha nia kwa kufika ofisi za Shirika la Nyumba la Taifa ili kuelezwa taratibu pamoja na hatua nyingine za kufanya kabla ya zoezi la uuzaji nyumba kuanza.

Mkurugenzi wa Ujenzi wa Shirika la Nyumba la Taifa ( NHC) Mhandisi Haikamen Mlekio alisema shirika lake kwa sasa liko hatua za mwisho za ukamilishaji mradi wa nyumba hizo 300 katika eneo la Iyumbu na kuongeza kuwa kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati watafanya kazi usiku na mchana ili mradi uishe kwa wakati.

Aidha, Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi amelitaka Shirika la Nyumba la Taifa kuongeza kasi katika ujenzi wa mradi huo wa Iyumbu na kusisitiza kuwa, mradi huo lazima uwe katika viwango vinavyotakiwa kwa kuzingatia sheria na taratibu za kimazingira.

‘’Ninyi ni waendelezaji kiongozi na wanaokuja wote waelewe kiwango cha kazi za NHC na viwango vyenu viwe vimekidhi mahitaji na kuzingatia sheria na taratibu zikiwemo za kimazingira ili wengine waje kujifunza na lazima kila kinachofanyika kiende katika utaratibu na Wizara ijivunie kuwa na shirika’. Alisema Dkt Mabula