Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) imesema video inayosambaa mitandaoni ikimuonyesha daktari aliyemshona jeraha mgonjwa na kufumua mshono kwa madai ya kushindwa kulipa gharama ni tukio lililotokea Julai, 2021.

Imesema lilitokea katika kituo cha afya Kerenge kilichopo tarafa ya Magoma halmashauri ya Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga.

Ufafanuzi huo umetolewa leo Jumamosi Septemba 4, 2021 baada ya kusambaa kwa video hiyo na kuzua mjadala mtandaoni huku Wizara ya Afya ikitoa tamko na kuomba mwenye kufahamu eneo husika kutoa taarifa na kisha kuweka namba ya simu.

Naibu katibu mkuu Tamisemi anayeshughulikia afya, Dk Grace Magembe amemtaja mtumishi aliyekiuka miiko ya udaktari kuwa ni Dk Jackson Meli ambaye ni ofisa wa kituo hicho cha umma.

“Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo ameshachukua hatua kwa kumsimamisha kazi na amempa hati ya mashtaka na pia ameshafikishwa kwenye baraza la madaktari ili achukuliwe hatua stahiki kwa kwenda kinyume na miiko ya taaluma ya udaktari,” amesema Dk Magembe.

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Korogwe, Mkoa wa Tanga, Halfani Magani amemsimamisha kazi Tabibu wa Zahanati ya Kerenge, Jackson Meli baada ya kufumua mshono wa mgonjwa Bi. Zubeda Ngereza kufuatia mgonjwa huyo kushindwa kulipa pesa za matibabu kiasi cha Tsh 10,000.

Magani amesema mtuhumiwa huyo ambaye amekamatwa na Jeshi la Polisi kwa mahojiano na uchunguzi, atafikishwa mahakamani kwa kosa la kukiuka maadili ya utabibu na kanuni za utumishi wa umma.