Jarida la Wall Street limeripoti kuwa Korea Kaskazini imekataa karibu dozi milioni tatu za chanjo ya Covid-19 zilizotengenezwa na kampuni ya Sinovac Biotech kutoka China. 

Kulingana na shirika linalosambaza chanjo kwa niaba ya mpango wa COVAX, taifa hilo limesema chanjo hizo zinastahili kupelekwa kwa nchi zilizoathirika vibaya zaidi na virusi vya corona. 

Mnamo mwezi Julai, Korea Kaskazini ilikataa chanjo za Astrazeneca kutokana na hofu ya madhara yake. 

Nchi hiyo iliyojitenga pakubwa kimahusiano na nchi zengine ulimwenguni, haijatangaza visa vyovyote vya maambukizi ya virusi vya corona na imeweka hatua kali za kudhibiti maambukizi ya virusi hivyo, ikiwemo kuifunga mipaka yake na kuzuia usafiri wa ndani ya nchi.