Mkurugenzi wa Kampuni ya VIP na aliyekuwa mmiliki mwenza wa IPTL, James Rugemalira aliyekuwa akikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi ameachiwa huru katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu baada ya Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali (DPP) kuifuta kesi hiyo.
 
Hatua hiyo inatokana na Mkurugenzi wa Mashataka nchini (DPP) kueleza kuwa hana nia ya kuendelea na shauri hilo dhidi ya mshtakiwa huyo.
 
Rugemalira na mwenzake, Harbinder Sethi walikuwa wakikabiliwa na mashtaka 12 yakiwemo ya uhujumu uchumi na utakatishaji fedha na kuisababishia Serikali hasara ya takribani shilingi bilioni 358.

Walifikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza Juni 19 mwaka 2017 ambapo makosa hayo walidaiwa kuyatenda Novemba 29 mwaka 2013 katika Benki ya Stanbic tawi la Kati Kinondoni.

Aidha, awali kulikuwa na mazungumzo na ofisi ya DPP ili kukubaliana namna ya kulipa fidia ili waachiwe, lakini baadaye mazungumzo hayo yalivunjika.

Juni 16 mwaka huu Seth aliachiwa huru kwa masharti ya kutotakiwa kutenda kosa lolote kwa kipindi cha mwaka mmoja, huku pia akitakiwa kulipa fidia ya shilingi bilioni 26.9 kwa Serikali ya kuingia makubaliano na DPP ya kumaliza kesi ya uhujumu uchumi iliyokuwa inamkabili kwa njia muafaka