Adeladius Makwega,WHUSM-Dodoma
Serikali imesema kuwa pale yanapotolewa maelekezo ya Serikali, mkuu wa taasisi ana wajibu wa kutekeleza maagizo hayo na siyo vingenevyo, kama mtu amechoka ni vizuri kuachia ngazi mara moja.

Kauli hii ya Serikali imetolewa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo mheshimiwa Innocent Bashungwa wakati akizungumza na menejiment ya wizara yake iliyowakutanisha wakuu wa Idara, vitengo na taasisi kadhaa zilizo chini yake.

“Mimi na naibu wangu sasa tumeshafanya kazi kwa muda na tunawatambua vizuri kama tunakuja kuitembelea taasisi yako tunatoa maagizo hauyatekelezi, tunarudi tena tunakuta hali ile ile sasa unataka nini kwetu, mimi na naibu wangu hatuwezi kuvumilia hali hii, naomba uondoke  kabla hatujafanya maamuzi hayo,”

Wizara yetu itafanyika vizuri sana kama maagizo ya serikali yanatekelezwa kwa wakati na anapokuja kiongozi mnaanzia pale  mlipotekeleza kwa agizo la awali na kundelea  mbele zaidi na serikali iweze kutoa maagizo mapya.

 “Wale ambao wanaojiona hawatoshi ondokeni haraka, mimi sitaki kuona hali ya utendaji kazi inakuwa hivyo, msilazimishe nichukue maamuzi ya haraka.” Aliongeza Waziri Banshungwa.

 Bahati kubwa wizara yetu kuwa na Msemaji wa Serikali na Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo ili aweze kufanya kazi vizuri anahitaji kupewa ushirikiano na idara zote za wizara hii na wizara zingine.

“Ninakupongea kwa kazi unayofanya, tangu uje na umeendelea kutoa ushauri wa hili na lile katika kazi zetu husasani za utoaji wa habari kwa umma, hongera kwa kazi nzuri.” Alisema.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo alisema kuwa lazima kazi zifanyike kwa umakini mkubwa kwani zinapofanyika vizuri ni sifa ya kila mmoja.

 “Kazi zote zifanyike ili kuepusha makosa yasiyo ya lazima na panapokuwepo na makosa inatoa ishara ya namna ya mtu aliyefanya kazi  hiyo alivyo.” Alisema Mhe Gekul.