SERIKALI kupitia Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia, Wazee na Watoto imesema mpaka kufikia jana Agosti 14, jumla ya walengwa 207,391 wamepatiwa chanjo ya kukinga maambukizi ya Uviko-19.

Takwimu hizo zinaonyesha wanaume wamechanjwa kwa asilimia 58.3 sawa na 121,002 na 86,389 wakiwa ni wanawake sawa na asilimia 41.7.

Taarifa iliyotolewa  Agosti 15, 2021 na Katibu Mkuu Wizara ya afya, Profesa Abel Makubi kuhusu maendeleo ya utoaji wa chanjo ya Covid-19 kwa wananchi imeeleza kuwa Serikali inaendelea kuratibu utoaji wa chanjo hiyo kupitia vituo vya kutolea huduma za afya vya umma na binafsi 550 vilivyoidhinishwa hapa nchini.