Wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) waliokuwa wamekusanyika nje ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu baada ya kuzuiwa kuingia ndani wanashikiliwa na Jeshi la Polisi.

Wafuasi  hao waliokuwa wamefika kwaajili ya kufuatilia kesi ya mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe ambaye hata hivyo hakufikishwa mahakamani walikamatwa baada ya kutoa mabango yenye jumbe mbalimbali na kuanza kuimba.

Baada ya wanachama hao kuanzisha nyimbo hizo, Polisi waliokuwa ndani ya magari wakiwa na silaha mbalimbali waliteremka na kuanza kuwakamata.

Kesi hiyo inayomkabili Mbowe na wenzake, ilikuwa inasikilizwa mahakamani hapo kwa njia ya mtandao ‘Video Conference’, mbele ya Haki Mkazi Mkuu, Thomas Simba, lakini baadae iliahirishwa  hadi kesho kutokana na tatizo la mtandao.