Marekani imesema imeizuia gari iliyokuwa imebeba shehena ya vilipuzi kwa kuishambulia kutoka angani ikiwa mjini Kabul hapo jana. 

Hayo yameripotiwa saa chache baada ya Rais wa Marekani Joe Biden kuonya kuwa kuna uwezekano wa kutokea shambulio lingine la kigaidi katika mji huo mkuu wa Afghanistan. 

Marekani imedai kuwa imeilenga gari pekee. Lakini vyombo vya habari vya Afghanistan vimeripoti kuwa kuna uwezekano raia pia wamejeruhiwa. 

Siku ya Alhamisi, mshambuliaji wa kujitoa muhanga kutoka kundi linalojiita Dola la Kiislam IS aliwalenga wanajeshi wa Marekani waliokuwa wakizuia umati mkubwa wa watu kuingia uwanja wa ndege wa Kabul, wakijaribu kuikimbia nchi hiyo. 

Tangu Taliban kunyakuwa madaraka, takriban watu 114,000 wameshahamishwa.

-DW