Na Mwandishi Wetu, Dodoma
Wazee nchini wameshauriwa kutumia fursa ya chanjo dhidi ya ugonjwa unaosababishwa na Virusi vya Korona UVIKO 19 ili kuimarisha kinga ya miili yao kipindi hiki ambacho Serikali imewapa kipaumbele.

Wito huo umetolewa leo na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu wakati akizungumza na Wajumbe wa Chama cha Wanasheria wanawake Nchini TAWLA waliomtembelea ofisini kwake jijini Dodoma.

Dkt. Jingu amesisitiza kuwa wakati huu ambapo  Dunia inapambana na maambukizi ya UVIKO 19 makundi mbalimbali yanatakiwa kushiriki kikamilifu kuhakikisha janga hilo.

“Kupitia mabaraza ya Wazee, wawahamasishe Wanachama wao kujitokeza kwa hiari kupata chanjo hiyo” alisema na kuongeza kuwa Wazee ni kundi ambalo lipo katika hatari zaidi ya kupata maambukizi ya UVIKO 19 hivyo Jamii ihamasishe Wazee wote kwenda katika vituo vya kutolea chanjo na kupata huduma hiyo amesisitiza Dkt. Jingu.

Ameongeza kuwa Wazee ni tunu ya Taifa hivyo Jamii ina wajibu wa kuwalinda na majanga mbalimbali ikiwemo kuimarisha usalama wa Afya zao.

“Uzee na kuzeeka unaambatana na changamoto ya kupungua kwa kinga ya mwili hivyo Serikali inatoa wito kwa Wazee wote nchini kujitokeza kutumia fursa ya chanjo ya UVIKO 19”  

Aidha, Dkt. Jingu amewataka Maafisa Ustawi na Maendeleo ya Jamii wote  kuhakikisha Wazee  wanaokwenda kupata chanjo kwenye vituo katika maeneo yao wanapata huduma zote wanazostahili bila usumbufu wa aina yoyote.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan alizindua mpango wa Chanjo hapa nchini  tarehe 28 Julai, 2021.