Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Kawe, Josephat Gwajima, amekanusha taarifa zilizokuwa zikisambaa mtandaoni zikidai kuwa amelishwa sumu kutokana na msimamo wake kuhusu chanjo ya Uviko-19.
 

Askofu Gwajima akizungumza kwenye ibada kanisani kwake Jijini Dar es Salaam amesema kuwa haitotokea mtu yeyote kumnywesha sumu katika siku za karibuni na wala serikali haiwezi kumnywesha sumu.

“Wanataka kusingizia watu, labda kusingizia kwamba serikali imeninywesha sumu, hakuna serikali iliyomnyeshwa sumu Gwajima kwa sababu serikali yenyewe ilisema kuchanja ni hiari kwa hiyo serikali haiwezi kumnywesha sumu mtu wala sijanywa sumu wala hakuna wakuninywesha sumu haitokeo leo wala kesho wala wiki ijayo katika jina la Yesu," amesema Askofu Gwajima.

Akijibu madai juu ya cheti kilichokuwa kikisamabazwa mtandaoni kuonyesha kuwa Askofu huyo ameshapata chanjo hivyo anawadanganya Watanzania, amesema kwamba cheti kile ni cha kufoji na hata aliyefoji ni dhahiri kuwa haujui Kingereza kwani badala ya kuandika 'certificate' ameandika 'certicate'.

Aidha, Gwajima amesisitiza kuwa kila mwanachi anao wajibu wakulinda afya yake .

Credit:Mwananchi