Na. Angela Msimbira KATAVI
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Ummy Mwalimu amewaagiza Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) Mkao Makuu kuacha kukaa 0fisini waende kwenye maeneo ya vijijini ili kuona changamoto na ubora wa barabara.

Ametoa agizo hilo leo alipotembelea na kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika kata ya Katuna, Halmashauri ya Wilaya Tanganyika Mkoani Katavi kwa lengo la kujua changamoto zinazozikabili Halmashauri zilizopo pembezoni.

Waziri Ummy alifafanua kuwa TARURA makao makuu wanatakiwa kutoka ofisini watembelee vijijini kujua maeneo ambayo yanachangamoto ya miundombinu ili kuweza kutoa vipaombele zaidi wakati wa kupanga bajeti za utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa barabara nchini.

“Haiwezekani TARURA mkakaa ofisini wakati matatizo mengi yanapatikana kwa wananchi hasa wale wanaokaa pembezoni, nawaagiza kuanzia sasa waache kukaa ofisini watoke na kwenda ‘site’ kujua changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi hasa katika maeneo ya vijijini,” alisisitiza Waziri Ummy

Alisema kwa sasa Serikali imejiwekea mkakati wa kuhakikisha inatatua changamoto za miundombinu ya barabara vijijini.
Alielieleza kuwa haiwezekani kukaa ofisini na kugawa fedha bila kujua changamoto za maeneo husika kwa sababu haki itakuwa haitendeki kwa baadhi ya Mikoa ambayo mtandao wao wa barabara ni mkubwa.

“Tumegundua kuwa kuna baadhi ya Halmashauri atuzitendei haki kwa kuwa mtandao wa barabara za TARURA haufiki hata kilometa 200 lakini kuna maeneo ambapo mtandao wao wa barabara ni zaidi ya kilometa 1900. Sasa unaposema Halmashauri zote zipate sawa hii si haki. Tunaenda kuzifumua bajeti za maendeleo ya ujenzi na ukarabati wa barabara ili kuziwezesha Halmashauri ambazo zinachangamoto kubwa” alisisitiza Waziri Ummy

Naye Mbunge wa Mpanda Vijijini Mhe Selemani Kakoso ameiomba Serikali kusaidia kujenga barabara ya kutoka Sibwesa – Kaduma yenye urefu wa kilometa 25 ambayo ipo katika mtandao wa TARURA.