Na. Hassan Mabuye, Pwani
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. William Lukuvi amemaliza mgogoro wa Ardhi kati ya mwekezaji wa Kampuni ya Dimara na  wakazi wa Kijiji cha Kisabi wilaya ya Kibaha mkoani Pwani uliodumu kwa zaidi ya miaka Saba.

 Waziri Lukuvi amemaliza mgogoro huo wakati akiwa katika ziara ya kutembelea maeneo yenye migogoro ya ardhi katika mkoa wa Pwani.

Akiwa katika Kijiji hicho Lukuvi alitoa maelekezo ya wavamizi wote waliojimilikisha sehemu ya eneo hilo kuondolewa na kupewa eneo katika shamba la ekari 51 lililorudishwa Serikalini hivi karibuni.

Lukuvi alitoa maelekezo kwa Halmashauri ya wilaya ya Kibaha kufufua mipaka ya eneo hilo na kuweka katika matumizi mazuri ya ardhi kupima viwanja na kuviuza kwa kushirikiana na mmiliki.

“sipo tayari kuwavumilia wavamizi kwenye maeneo yanayomilikiwa kihalali na nimeamua kuja Pwani kwakua mnaongoza kwa kuvamia maeneo bila kufuata sheria, kazi yangu ni kuwalinda wanaomiliju ardhi kisheria na kimila nataka nirudishe heshima” alisema Mhe. Lukuvi.

Alisema wananchi hao watapewa maeneo kwenye ekari 51 za shamba ambalo lilifutwa umiliki wake na Mhe. Rais na kurudishwa Serikalini na wanalazimika kulipa gharama za hati miliki baada ya viwanja kupimwa katika Halmashauri ya Kibaha.

Waziri Lukuvi pia alitoa maelekezo kwa wakuu wa mikoa na wilaya kutembelea maeneo yenye migogoro ya ardhi na kuondoa wavamizi ili kukomesha tabia hiyo.

Alitoa onyo kwa maofisa ardhi kuhakikisha wanapopeleka majina ya maeneo ambayo hayajaendelezwa kwa Waziri watende haki kwa kuwa na ushahidi kutoka kwa mkuu wa wilaya atakayekiuka hatua zitachukuliwa.

Mkuu wa Mkoa wa Pwani alizindua kampeni ya kutokomeza migogoro ya ardhi mapema wiki hii lengo kumaliza migogoro iliyopo na kukomesha uvamizi kwenye maeneo yanayomilikiwa kisheria katika mkoa huo.