Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. George Simbachawene amesema serikali inatambua umuhimu wa sekta ya usafirishaji nchini na kwamba pamoja na umuhimu huo pia serikali imeahidi kufanyia kazi changamoto zilizopo ikiwemo muingiliano wa kimamlaka kati ya Jeshi la Polisi na LATRA.

Waziri Simbachawene amesema hayo jana wakati akizungumza na wadau wa sekta ya usafirishaji nchini kwenye kikao kazi kilichofanyika jijini Dar es salaam na kuhusisha wadau mbalimbali katika sekta hiyo kwa lengo la kutatua changamoto zinazoikabili.

Kwa upande wake Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro amesema Jeshi hilo limeanza kushughulikia maombi kadhaa yaliyowasilishwa na wadau wa sekta ya usafirishaji ambapo kati ya maombi hayo ni pamoja na mabasi kuruhusiwa kutoka saa kumi na moja alfajiri sambamba na kuwepo kwa kituo cha maalum cha  ukaguzi katika stendi kuu ya mabasi iliyopo Mbezi jijini Dare s salaam.

Kwa upande wake mdau wa sekta ya usafirishaji amesema Jeshi la Polisi linajitahidi katika kutatua changamoto za usalama barabarani lakini ameelekeza kuwepo kwa changamoto kwa LATRA kwa kutotoa ushirikiano kwa wadau hao wa usafirishaji na hivyo kukwamisha baadhi ya mambo muhimu.