Serikali imesema haijatoa maelekezo ya kuwalazimisha watumishi wa umma kupokea chanjo ya Corona kama ambavyo imezushwa na wahalifu kupitia mitandao ya kijamii.

Kauli imetolewa jana Alhamisi Julai 29, 2021 na Msemaji wa Serikali, Gerson Msigwa katika taarifa yake kwa umma, akiwataka wananchi kupuuza uzushi huo.

Msigwa amewataka watumishi wa Serikali kuendelea kupokea taarifa rasmi kutoka Serikalini kupitia kwa viongozi pamoja na kuzingatia maelekezo yanayotolewa na wataalamu kuhusu  afua mbalimbali za kujikinga na Corona.

Amefafanua kuwa msimamo wa Serikali ni kuwa utoaji wa chanjo ya Corona unafanyika kwa hiari ya mtu yeyote atakayekuwa tayari kuipokea. Amesema makundi yatakayopewa kipaumbele ni watumishi wa afya na watu wenye magonjwa sugu.

 “Watu wenye umri wa zaidi ya miaka 50 na askari waliopo katika vyombo vya ulinzi na usalama.Serikali inawataka wanaofanya uhalifu huu wa kuwatisha wananchi kuacha mara moja kwa kuwa ni makosa kisheri,” amesema Msigwa.

Kwa mujibu wa Msigwa, kwa sasa Serikali inaendelea kukamilisha maandalizi ya kutoa chanjo hiyo, katika mikoa 10 itakayoanza kutoa huduma hiyo kwa wananchi na utaratibu wake utaelezwa baadaye.