Na Mwamvua Mwinyi,Pwani
MKUU wa mkoa wa Pwani ,Aboubakar Kunenge ametoa onyo kali kwa watu wanaojihusisha na uhalifu mbalimbali ikiwemo wizi, ubakaji, kuvamia nyumba za ibada,matumizi ya dawa ya kulevya na uingizaji wa wahamiaji haramu kuacha mara moja kwani kinachofuata ni kuchukuliwa hatua stahiki za kisheria.

Amewaasa viongozi wa dini kushirikiana na serikali kuwatangazia waumini wao juu ya kuacha vitendo hivyo viovu .

Akizungumza mjini Kibaha na viongozi wa madhehebu mbalimbali mkoani Pwani Kunenge alisema , wameshatoa matamko mengi kwa wananchi lakini baadhi ya watu bado wanaendelea kujihusisha na matukio hayo ambayo ni kero kwa wananchi.

“Tumetoa matamko mengi ya kuwataka watu waache kujihusisha na uhalifu lakini baadhi bado wanaendeleza vitendo hivyo lakini kwa sasa tumefika mwisho ,”alisema Kunenge.


“Serikali imekuwa ikijitahidi kutoa elimu na ushauri kwa wananchi kutojihusisha na vitendo vya uhalifu lakini bado wanaendeleza vitendo vya kihalifu .

Naye mwenyekiti mwenza wa kamati ya amani ya mkoa, Beno Kikudo alieleza baadhi ya watu wanakiuka maadili ya imani zao na kusababisha vitendo viovu kuendelea ndani ya jamii.


Kwa upande wake mwenyekiti mwenza wa kamati ya amani ya mkoa ,Sheikh Hamis Mtupa alisema kumekuwa na matukio mengi ya uhalifu ambapo baadhi wamekuwa wakivamia hata kwenye nyumba za ibaada.