Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Hussein Mwinyi amewasimamisha kazi Wakurugenzi wote wa halmashauri za wilaya za Unguja, baadhi ya Wakurugenzi wa Taasisi na Idara za Serikali, pamoja na Watendaji wengine waliobainika kuhusika na wizi, kutowajibika kazini na ubadhirifu wa mali za Serikali.

Dkt. Mwinyi ametangaza kuwasimamisha kazi Watendaji hao katika mkutano wa majumuisho baada ya kuhitimisha ziara yake katika mikoa mitatu ya Unguja.

Baadhi ya Watendaji waliosimamishwa kazi ni Wakurugenzi wa halmashauri za wilaya ya Mjini, Magharibi A na B, Kaskazini A na B, Kusini, wilaya ya Kati pamoja na Mkurugenzi wa SMIDA.
 
Akitangaza uamuzi huo, Dkt. Mwinyi  amewataka Watendaji wote wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kubadilika na kuacha kufanya kazi kwa mazoea.

Amesema kumekuwa na mikataba mingi ya kifisadi inayofanyika katika baadhi ya halmashauri za wilaya, na kutolea mfano halmashauri ya wilaya ya Mjini ambayo imeingia mikataba ya aina hiyo na kampuni za simu pamoja na mikataba katika uwekaji wa mabango.