Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema kuwa Serikali inathamini mchango wa Sekta Binafsi na Taasisi za Dini likiwemo kanisa Katoliki katika kuimarisha upatikanaji wa huduma mbalimbali za kijamii nchini.

Ametoa kauli hiyo jana (Jumapili Julai 4, 2021) alipomuwakilisha Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan katika ibada ya kuwekwa wakafu na kusimikwa kwa Askofu mpya wa Jimbo Katoliki la Bunda, Askofu Simon Chibuga Masondole. Ibada hiyo imefanyika katika viwanja vya Kanisa Kuu Bunda, Mkoani Mara.

Amesema kuwa Serikali kwa upande wake itaendelea kushirikiana na madhehebu ya dini katika kutoa huduma hizo kwa Watanzania wote bila ubaguzi wa aina yoyote.

"Upo usemi usemao “Kama unataka kwenda haraka tembea peke yako, lakini kama unataka kwenda mbali tembea na wenzako”. Sisi wote tuna imani kubwa nawe kuwa utaendeleza mashirikiano mazuri yaliyopo baina ya Serikali na Kanisa"

Aidha, Waziri Mkuu amewataka Watanzania kutumia nyumba za ibada kuliombea Taifa ili waendelee kuishi kwa amani, upendo na mshikamano.

"Amani tuliyo nayo, ndiyo chachu kubwa ya kufikia mafanikio ya maendeleo ya kijamii, kisiasa na kiuchumi"

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mara Ally Hapi amesema wataendelea kutoa ushirikiano usio na mashaka kwa askofu mteule na Kanisa Katoliki kwa kuwa wanatambua mchango wa Kanisa hilo katika mkoa wa Mara.

(Mwisho)
IMATOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU