Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa, Kassim Majaliwa Majaliwa kesho Juni 8, 2021 anatarajia kufungua Mashindano ya Michezo na Taaluma kwa Shule za Msingi (UMITASHUMTA) na Sekondari (UMISSETA) kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara.

Mashindano haya yanajumuisha mikoa yote kutoka Tanzania Bara na Visiwani ambapo yatafanyika kwenye viwanja vya Nangwanda Sijaona, Chuo cha Walimu Mtwara (TTC kawaida) Chuo cha Walimu Ufundi maarufu kama Mwasandube, na viwanja vya Shule ya Sekondari ya Ufundi Mtwara ambapo yanaanza kesho Juni 08, 2021 na kumalizika Julai 03, 2021. Mashindano yameandaliwa na Wizara tatu zinazohusika na Elimu, Habari na TAMISEMI chini ya Kamati ya Uratibu ya Kitaifa ya Makatibu Wakuu wa Wizara hizo.

Michezo itakayoshindaniwa kwa upande wa UMITASHUMTA ni mpira wa miguu kwa wasichana na wavulana, mpira wa miguu maalum kwa wavulana (wenye ulemavu wa kusikia) mpira wa pete, mpira wa goli kwa wasichana na wavulana wasioona na wenye uoni hafifu, mpira wa wavu kwa wasichana na wavulana, mpira wa mikono kwa wasichana na wavulana, mpira wa meza kwa wasichana na wavulana, riadha jumuishi, kwaya na ngoma.

Kwa upande wa UMISSETA michezo itakayochezwa ni yote ya UMITASHUMTA pamoja na mchezo wa mpira wa kikapu kwa wasichana na wavulana isipokuwa mchezo wa mpira wa goli, aidha kutakuwa na mashindano ya usafi katika mazingira wanayoishi. Mashindano yatapambwa na wasanii wa kizazi kipya kama Ibrah kutoka Konde Gang, Beka Flavour, Dulla Makabila, Linah Sanga na Peter Msechu na kwa upande wa taarabu Mzee Yussuf pia atakuwepo ili kutoa hamasa na burudani. Pia vyama vya michezo, mashirikisho na vilabu vya michezo mbalimbali vimealikwa kuja kuangalia vipaji mbalimbali.