Na.Catherine Sungura,Dodoma
Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imesisitiza miongozo yote iliyotolewa kwa umma kujikinga dhidi ya maambukizi ya Virusi vya CORONA (COVID – 19), izingatiwe.

Mkurugenzi wa Idara ya Kinga wa Wizara hiyo, Dkt. Leonard Subi amesema Tanzania ni salama hata hivyo kwa kuwa bado kuna tishio la maambukizi ya Virusi hivyo duniani, ni muhimu kuendelea kuchukua tahadhari za kujikinga.

Dkt. Subi amesema hayo leo alipohojiwa na moja ya chombo Cha habari jijini Dodoma ni hatua gani Tanzania inaendelea kuzichukua kuhakikisha jamii inakingwa dhidi ya wimbi jipya la maambukizi ya COVID – 19.

“Tanzania tupo salama lakini tunatakiwa kuendelea kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi hayo ambayo kwa takriban mwaka na nusu sasa bado yanaikabili dunia.

“Wizara kazi yetu ni kuendelea kihimiza wananchi kujikinga dhidi ya COVID – 19, tuendelee kuchukua tahadhari, tuliona katika wimbi la kwanza 2020 wananchi waliitika wito wa kunawa mikono, kuvaa barakoa, kukaa umbali, kufanya mazoezi, lishe bora na masuala mengineyo,” amesema.

Ameongeza “Tunataka kusisitiza kinachotokea Afrika maambukizi yanaongezeka na baadhi ya Wakuu wa Nchi wanatoa matamko kama tulivyomsikia Rais wa Uganda na sisi Tanzania tumekuwa na mwingiliano na uhusiano mwema na nchi jirani.

“Watanzania kinga ni bora kuliko tiba tusije tukasubiri kuingia kwenye mitungi ya oksijeni, tuendelee kujikinga. Hali ni shwari hata Rais Samia Suluhu Hassan anachukua tahadhari kujikinga na maambukizi akikutana na watu mbalimbali,” amesema.

Amesisitiza “Mashuleni, vituo vya afya tuliweka vifaa kwa kunawa kwa maji safi tiririka, tunawe mikono.

Akitolea mfano wa Ma-benki kwenye ‘ATM’ waliweka vipukusi ‘sanitizers’, Ila Kwenye ATMs sasa hivi havipo na watu wanashika wanabonyeza bonyeza pale inaweza kuwa chanzo cha maambukizi.Alizitaka benki zote wahakikishe wanarejesha vitakasa mikono na kuwapa siku tatu.

“Hatua tulizopiga tusije tukarudi tulipotoka, sisi Serikali tunaendelea kufuatilia kwenye mikusanyiko, mabasi, ndege wachukue tahadhari.

Amesema Serikali imeimarisha hatua za ufuatiliaji kwenye maeneo ya mipaka, viwanja vya ndege watu wanapimwa hali zao za afya.

“Tunafahamu kuna tishio kubwa la anuwai mpya (aina mpya ya kirusi cha CORONA) duniani, kuna cha India, Uingereza, Afrika Kusini na Brazil ambavyo vimeendelea kugharimu maisha ya watu.

“Tunashirikiana na Mamlaka za mikoa, Serikali za Mitaa kuhakikisha tunaendelea kuwafikia wananchi,” amesema.

Dk. Subi pia ametoa rai kwa vyombo vya habari kuendelea kuelimisha jamii na kuihamaisha kujikinga dhidi ya maradhi hayo.

“Tunaomba vyombo vya habari mtumie muda wenu kidogo hata mara moja au mbili kwa siku kuwakumbusha wananchi kuchukua tahadhari juu ya COVID – 19.

“Suala la mapambano dhidi ya magonjwa si la hiyari, tuna maafisa afya pia, Watanzania suala la afya ni la muhimu na la msingi kwa Maendeleo ya Taifa tukicheza tutarudi nyuma, kila mmoja atimize wajibu wake.

“Kwenye familia ndoo za kunawa mikono kwa maji tiririka na sabuni ziwepo, bebeni vipukusi na katika maeneo ya mikusanyiko tunashauri barakoa zivaliwe kwa kuzingatia mwongozo tuliotoa na kwenye nyumba, magari kuwe na mzunguko wa hewa, tujikinge,” ametoa rai Dk. Subi.