Na. Saidina Msangi na Peter Haule, WFM. Dodoma
Serikali imefungua wigo kwa sekta binafsi kushiriki katika utekelezaji wa miradi ya kimkakati ili kufanikisha utekelezaji wa malengo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano 2021/22-2025/26 unaotarajiwa kuzinduliwa hivi karibuni.

Hayo yameelezwa jijini Dodoma na Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), alipokutana na wadau na taasisi za fedha nchini katika kikao kilichoangazia ugharamiaji wa miradi ya maendeleo kwa njia mbadala.

Akizungumza katika kikao hicho Mhe. Dkt. Nchemba alisema kuwa tathmini iliyofanyika ya utekelezaji wa Mpango wa Pili wa Maendelo wa Taifa ilibainisha ushiriki mdogo wa sekta binafsi katika utekelezaji wa mpango huo hivyo Serikali imeona ijadiliane nao kuona namna bora ya kuwezesha ushiriki wa sekta binafsi katika Mpango wa Tatu wa Taifa wa Maendeleo.

“Tuliona tujadiliane tunapokwenda kuanza mwaka mpya wa fedha na tukijua tuna miradi ya kitaifa inayoendelea tuanze kwa pamoja kwa kuangalia njia mbadala tunazoweza kutumia kufanikisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo,”alisema Mhe. Dkt. Nchemba.

Alisema kuwa kuna umuhimu wa kuwa na njia mbadala za kuwezesha utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo ili isiathiri utekelezaji wa shughuli za utoaji wa huduma za kijamii, ikiwemo elimu, maji na afya.

Alifafanua kuwa kwa upande wa miradi inayoweza kutekelezwa kwa njia mbadala Serikali itaboresha mazingira ya kuwezesha utekelezaji wa miradi hiyo kupitia sekta binafsi kwa kuhakikisha inafanyia kazi baadhi ya hoja zilizoibuliwa katika kikao hicho ikiwemo masuala ya kiutawala.

Akizungumza wakati akimkaribisha Waziri wa Fedha na Mipango, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo na Bw. Emmanuel Tutuba alisema kuwa Serikali imeshirikisha sekta binafsi ili kupata fedha nyingi zaidi kwa ajili kutekeleza miradi ya maendeleo kwa wakati.

Alisema kuwa Serikali inatarajia mchango mkubwa kutoka sekta binafsi katika utekelezaji wa Mpango wa Maendelo wa Taifa wa Tatu na kuwa itaendelea kupokea maoni na mawazo kutoka sekta binafsi ili kuwezesha utekelezaji wa miradi mingi zaidi.

“Nitoe wito kwenu kuwasilisha wizarani maeneo mnayohitaji maboresho ya kisera na kikodi ili yaweze kufanyiwa kazi kwa mujibu wa sheria ili kufanikisha ushiriki wenu kikamilifu katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo,” alisema Bw. Tutuba.

Aidha Bw. Tutuba ametoa wito kwa wadau hao kutoa ushirikiano kwa Serikali na kukaribisha wawekezaji kutoka nje ili nao waweze kuona maeneo wanayoweza kushiriki katika utekelezaji wa miradi mikubwa na midogo iliyo katika mpango huo.

Naye Kamishna wa Idara ya Uendelezaji wa Sekta ya Fedha Dk. Charles Mwamwaja alisema kuwa dirisha hilo litatoa fursa kwa Serikali kupata fedha kutoka vyanzo vya ndani kutatua changamoto ya upatikanaji wa fedha za miradi na kuharakisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo itakayojumiisha maeneo mengi zaidi.

“Mpango huo utasaidia katika kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa miradi ya maendeleo huku ikitoa fursa kwa Serikali kujielekeza katika maeneo mengine ya vipaumbele ambayo sekta inafsi haiwezi kufika,”alisema Dk. Mwamwaja.

Alifafanua kuwa Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa umebainisha kiwango cha fedha kitakachohitajika katika utekelezaji wa miradi ambapo Serikali inatarajia kukusanya kiasi cha Sh. trilioni 74.3 katika vyanzo vyake na kiasi cha Sh.40.6 kinatarajiwa kupatikana kutoka vyanzo mbadala ikiwemo Sekta Binafsi.

Kwa upande wa sekta binafsi, imepongeza hatua ya Serikali kufungua rasmi dirisha la ushiriki wa sekta binafsi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kubainisha kuwa wako tayari kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa mpango huo.

Wamepongeza pia uamuzi wa Serikali wa kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara na uwekezaji hatua inayiwapa Imani ya kuwekeza mitaji na fedha zao katika ujenzi wa miradi hiyo yenye lengo la kuboresha maisha ya watu na kukuza uchumi wa nchi.