Samirah Yusuph
Simiyu.
Mkuu wa mkoa wa Simiyu David Kafulila ameagiza uhakiki wa kiasi cha madini ya ujenzi yanayotoka katika kila halmashauri za wilaya ya mkoa huo kwenda katika ujenzi wa barabara na miradi mingine.

Agizo hilo amelitoa  Juni 1,2021 alipo kuwa katika ukaguzi wamradi wa ujenzi wa Barabara ya Bariadi, Mwigumbi yenye urefu wa kilometa 50.3 kufuatia uwepo wa halmashauri za wilaya ambazo hazifahamu thamani ya malipo ya madini hayo.

Kafulila ameagiza kuwa kila halmashauri kufanya uhakiki wa kiasi cha madini ambayo yamechimbwa kwa kipindi cha miaka mitano na kupata thamani yake ili mkandarasi aliyehusika na uchimbaji huo afanye malipo.

"Halmashauri zote ndizo zenye mamlaka ya kutenga maeneo ya kuchimba madini ya ujenzi na walipwe ushuru wao, ili pesa ya Mrahaba na asilimia moja ya ukaguzi iende tume ya madini...Ile dhana ya mtu kuendelea kuvuna kokoto kwa leseni ya Tanroad baada ya kuwa mradi umekamilika iwe ni mwisho".

Aidha ameongeza kuwa hadi sasa Tume ya madini mkoa wa Simiyu inadai tsh670 milioni za mirahaba ya madini kwa mkandarasi wa barabara hiyo huku pesa iliyolipwa kwa kipindi chote hicho ikiwa ni tsh 20 milioni pekee huku halmashauri ya wilaya ya Maswa yalipo machimbo ya kokoto hizo haifahamu ni kiasi gani inatakiwa kulipwa.

Jambo ambalo mkurugenzi wa wilaya hiyo Dkt Fredrick Sagamiko ameelezea kuwa licha ya halmashauri kufuatilia kwa ukaribu zoezi la uchimbaji wa madini hayo kwa kipindi chote hawakuweza kupewa ushirikiano na  wakala wa barabara (tanroads) ambaye ndiye mwenye mkataba na mkandarasi.

Katika hatua nyingine Kafulila amewatahadharisha wakandarasi wanaofanya kazi chini ya kiwango katika  mkoa huo kuwa hakuna nafasi ya kuwavumilia tena huku akimtaka mkandarasi anayejenga kipande hicho cha barabara kufanya kazi kwa weredi baada ya kazi ya awali kulazimika  kuirudia kutokana na kuwa ilijengwa chini ya kiwango ujenzi ambao umeanza tangu 2015 hadi sasa haujakamilika.  

Mwisho.