Rais Samia Suluhu Hassan ameusimamisha kwa muda  uongozi wa soko la Kariakoo lililopo jijini Dar es salaam, na kuagiza uchunguzi ufanyike kuhusu tuhuma mbalimbali zinazoukabili uongozi huo.

Rais Samia Suluhu Hassan ametangaza hatua hiyo wakati wa ziara yake ya kushtukiza katika soko hilo, ambapo pia amesikiliza kero za Wafanyabiashara mbalimbali wa soko hilo.

Amesema hali ya soko hilo la Kariakoo hairidhishi, na kwamba Serikali kwa sasa inaenda kufanya tahmini ya kina kuona namna ya kuliendesha soko hilo.

Rais Samia Suluhu Hassan amesema lengo la kuanzishwa kwa soko hilo ni kuwasadia Wafanyabiashara wadogo, lakini kwa sasa jambo hilo halipo na kinachofanyika ni kuwanufaisha viongozi wa soko hilo pekee.

Ameongeza kuwa mpangilio wa bidhaa ndani ya soko hilo ni mbaya, jambo ambalo linahitaji kufanyiwa marekebisho ya haraka.