Idara ya sheria ya Marekani imesema mamlaka nchini humo imezifungia tovuti za habari zenye mafungamano na serikali ya Iran kwa tuhuma za kueneza habari za upotoshaji.

Idara hiyo imesema tovuti 33 zilizofungiwa zilitumiwa na vituo vya redio na televisheni ya serikali ya Iran, vituo ambavyo serikali ya Marekani inavituhumu kwa kueneza habari za uwongo na zenye nia ya kuwapotosha wapiga kura wa Marekani kabla ya uchaguzi wa rais wa mwaka 2020.

Marekani imesema tovuti tatu kati ya hizo zilikuwa zinaendeshwa na kundi la Kata'ib Hizballah, ambalo zaidi ya muongo mmoja uliopita lilitajwa kuwa kundi la kigaidi.Kundi hilo ni tofauti na lile la wanamgambo wa Hezbollah ambalo tovuti zake za habari zinaendelea kufanya kazi.

Tangazo la Marekani linajiri saa chache tu baada ya shirika la habari la serikali ya Iran IRNA kusema, Marekani ilizifunga tovuti za Iran bila ya kutoa maelezo zaidi.