Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro amewataka wadau wa usafirishaji kuendelea kushirikiana na Jeshi hilo na kutoa mchango wao utakao saidia kupunguza ajali zinazosababisha vifo na majeruhi kwa watumiaji wa vyombo vya usafiri.

IGP Sirro amesema hayo leo jijini Dar es salaam wakati akizungumza na wadau wa usafirishaji nchini katika kikao kazi cha kufanya tathimini, changamoto na mafanikio kwa kipindi cha mwaka mzima.

Aidha, IGP Sirro ametoa maagizo kwa Makamanda wa Polisi nchini kuhakikisha wanafanya ukaguzi wa magari katika maeneo yaliyoainishwa na kuepuka kusimamisha magari mara kwa mara.

Naye mdau wa usafirisha bwana Enos Lema, ameiomba serikali pamoja na mamlaka zinazohusika kuangalia upya suala la mabasi ya abiria yanayofanya safari zake mikoani pamoja na nchi jirani kuruhusiwa kuanza safari hata nyakati za mchana hatua itakayowezesha kupunguza changamoto za usafirishaji kwa abiria.