Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt.Damas Ndumbaro aahidi kutumia ushawishi wake kuwahamasisha Mawaziri wenzake pamoja wa watu kawaida  kujifunza mchezo wa gofu kufuatia ombi la Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania, Mhe.Frederic Clavier kufanya hivyo

Ametoa kauli hiyo jana wakati wa hafla ya kutoa zawadi kwa Mabalozi na Wataalamu wa nchi mbalimbali ambao ni Wachezaji na Wanachama wa Chama wa gofu nchini kufuatia kumalizika kwa mashindano ya Gofu  yaliyoandaliwa na Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania yaliyofanyika Mwezi April mwaka huu Jijini Dar es Salaam.

 Hafla hiyo ya utoaji zawadi kwa Wachezaji wa gofu imefanyika nyumbani kwa Balozi huyo, Mhe.Frederic Clavier  na kuhudhuriwa na Mabalozi na Wataalamu mbalimbali wanaoziwakilisha nchi zao nchini Tanzania  ambao ni Wachezaji wa Gofu na Wanachama wa Gofu nchini Tanzania.

Amesema kufuatia ombi la Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania, Mhe.Frederic Clavier mbali ya kuwahasisha Mawaziri pia atawahamasisha Wabunge kujifunza mchezo huo ili kuwa timu bora ya Bunge ya mchezo wa gofu  hali itakayopelekea Wabunge hao kuendeleza mchezo huo katika majimbo waliyotoka.

Akizungumza katika hafla hiyo, Waziri Dkt.Ndumbaro amewapongeza Washiriki hao na kuwaaahidi kuendeleza mchezo huo kwa kuunganisha na utalii wa michezo ili kuhamasisha Mabalozi hao kutembelea vivutio vya Utalii vilivyopo nchini.

‘” Nawaahidi  kuandaa mashindano mengi zaidi ya Gofu ambayo nitawashirikisha karibu  vivutio vya Utalii ili mkishacheza gofu mbajipumzisha kwa kuwa tembo na simba” alisema Ndumbaro

Kwa upande wake Balozi wa Ufaransa nchini Tanzania, Mhe. Frederic Clavier ametoa wito kwa Watanzania kujifunza mchezo wa gofu huo kwani ni mchezo kama michezo mingine

Amewatoa hofu Watanzania kuwa mchezo huo haubagui ni wa watu wote wenye kipato cha chini na cha juu na sio mchezo wa Watu wa Matajiri na Wasomi  pekee

Amesema gofu ni mchezo rahisi sana kujifunza na sio mchezo mgumu, ” Jitokezeni kujifunza mchezo wa Gofu ni ajira na pia ni burudani kama ulivyo mchezo wa mpira wa miguu” alisema Mhe.Balozi Frederic Clavier

Katika hatua nyingine amempongeza Waziri Dkt. Ndumbaro kwa kuwa Mwanachama pekee wa Mchezo wa Gofu kati ya Mawaziri wote nchini Tanzania na hivyo kutoa wito kwa Mawaziri wengine kucheza mchezo huo.