Vijana wanaojishugulisha na kilimo hai kwenye wilaya ya Chamwino mkoa wa Dodoma wameiomba serikali iwasaidie kupata uhakika wa masoko ya mazao yao ikiwemo alizeti, mahindi, kunde, ufuta na mazao ya mboga mboga.


Wamaetoa ombi hilo jana Jumamosi (01.05.2021) wakati wataalam wa Wizara ya Kilimo wanaofanya ufuatiliaji wa utekelezaji wa Mkakati wa Taifa  Vijana kushiriki kwenye sekta ya Kilimo (NYSA) kuzalisha ajira  walipotembelea vikundi sita vya vijana.


“Tunalima mboga mboga mboga pia alizeti hapa kijijini lakini changamoto yetu imekuwa uhaba wa masoko ya mazao yetu hali inayopunguza morali ya vijana kuendelea na kazi za Kilimo” alisema Christopher Joseph kijana mjasiliamali


Akizungumzia kuhusu kazi zilizofanywa na shirika la Kilimo Endelevu (SAT) linalotekeleza mradi wa Wanawake Dodoma katika Maendeleo ya Kilimo na Biashara (DWABI) Mratibu wake Elizabet Kilia alisema jumla ya vijana 2,563 kati yao wasichana 2,354 na wavulana 209 wamefikiwa na kuunganishwa kwenye vikundi vya kilimo hai (organic farming).


Aliongeza kusema jumla ya vikundi 90 katika wilaya za Chamwino, Mpwapwa na Dodoma wamefikiwa na elimu ya kilimo hai na ujasiliamali kupitia shirika la SAT ambapo linalenga kuboresha maisha ya vijana hususan akina mama wadogo (young mothers) kiuchumi kupitia kilimo ambao wamezaa mapema wakiwa na umri mdogo .


Elizabet  alisema kwa upande wa ujasiliamali jumla ya vijana 1,900 wamejengewa uwezo kwenye ujasiliamali kwa nadharia na vitendo kuweza kutengeneza bidhaa za  kijasiliamali kama batiki, kuongeza thanani ya zao la ubuyu, sabuni za maji na mikoba ya shanga,


Naye Mratibu wa Mkakati wa Vijana Kushiriki katika Kilimo toka Wizara ya Kilimo aliyeongoza tumu ya wataalam kukagua miradi ya Vijana Revelian Ngaiza aliwapongeza vijana wa Chamwino kwa ubunifu wao uliokuza uzalishaji wa mazao hali ilisaidia kubaidilisha maisha yao kwa kuwa na uhakika wa kipato kwenye kaya .


Ngaiza aliongeza kusema suala la uhaba wa masoko kwa mazao ya kilimo ni agenda kuu ya serikali ya awamu ya sita ambapo mikakati imewekwa ili kuwezesha wakulima wapate masoko na kuuza mazao yao, hivyo amewataka vijana kutokata tamaa bali waendelee kujishughuli kazi za kilimo ikiwemo za uongezaji thamani mazao ya kilimo na mifugo.


“Rais Samia Suluhu Hassan tayari ameshatoa maagizo kwa wizara ya Kilimo na ile ya Viwanda na Biashara kuhakikisha mazao ya wakulima yanapata masoko ya uhakika .Agizo hilo alilotoa wakati akihutubua Bunge huvu karibuni, hivyo vijana endeleeni kulima kwa kuzingatia tija na soko litapatikana” alisisitiza Ngaiza.


Kuhusu changamoto ya vijana kupata ardhi na kuondokana na gharama kubwa ya kukodi Ngaiza alitoa wito kwa Halmashauri nchini kote kutenga ardhi maalum kwa ajili ya vijana kwenye vijiji ili waweze kuzalisha mazao ya Kilimo na kuwa na uhakika wa ajira na kipato hatua itakayosaidia utekelezaji wa mkakati wa Taifa kuhusu vijana kushiriki kwenye sekta ya Kilimo.


Kwa upande wake Mkurugenzi wa shirika la Kilimo Endelevu (SAT) Janet Maro alisema wapo tayari kununua mazao yote ya vijana yaliyozalishwa kwa njia ya Kilimo hai msimu huu ikiwemo alizeti, karanga, ufuta, mahindi na mpunga.


Katika kuhakikisha vijana wanawezeshwa na kusimamiwa kuzalisha mazao kwa njia ya Kilimo hai SAT tayari imefanikiwa kutoa mafunzo kwa maafisa ugani 40 toka wilaya za Chamwino (19),Dodoma (1) na Mpwapwa (20) mafunzo yaliyotolewa kwenye kituo cha mafunzo Vianzi mkoani Morogoro mwaka 2020.


Mwisho.