Serikali imepiga marufuku wanafunzi wanaoanza elimu ya msingi (darasa la kwanza) kudaiwa vyeti vya elimu ya awali, kwa maelezo kuwa hakuna sera inayoelekeza shule za awali kutoa vyeti hivyo.

Marufuku hiyo imetolewa na Waziri wa TAMISEMI, Ummy Mwalimu bungeni mjini Dodoma leo wakati akitoa jibu la nyongeza kufuatia swali lililoulizwa na Mbunge Mariamu Kisangi ambaye alitaka kujua kutokana utaratibu wa vyeti hivyo kutakiwa, serikali ina mpango gani kuhakikisha elimu hiyo inatolewa kwa wanafunzi wote.

"Mheshimia Spika,naomba nitoe tamko la kisera hapa...Ni marufuku shule kudai certificates  za awali kwa wanafunzi wanaoanza darasa la kwanza .Bado hatujafanya vizuri katika kuongeza access  ya watoto kuanza elimu ya awali. Kwa hiyo haileti mantiki kusema kila mtoto aanze darasa la kwanza awe na certificate ya awali,” amesema Waziri Ummy.

Hata hivyo ameahidi kuwa serikali itaweka nguvu kuhakikisha kuwa watoto wanapata elimu ya awali hususani katika maeneo ya vijijini.

Awali Naibu Waziri katika Wizara ya Tamisemi David Silinde alisema madai ya vyeti kwa wanafunzi wanaoandikishwa hudaiwa kwa shule binafsi lakini si utaratibu wa Serikali.