Rais Samia Suluhu Hassan ameondoka nchini kuelekea nchini Kenya, kuanza ziara ya kikazi ya siku mbili kwa mwaliko wa Rais Uhuru Kenyatta wa nchi hiyo.

Akiwa nchini Kenya, Rais Samia Suluhu Hassan atakuwa na mazungumzo na mwenyeji wake Rais Kenyatta na kisha atalihutubia Bunge la nchi hiyo litakalojumuisha Wabunge wa Mabunge yote mawili ya nchi hiyo.

Aidha, atahudhuria na kuhutubia mkutano wa jukwaa la Wafanyabiashara wa Tanzania na Kenya utakaofanyika jijini Nairobi.