Rais Samia Suluhu Hassan amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Mstaafu wa Nigeria, – Olusegun Obasanjo.

Mazungumzo hayo yamefanyika Ikulu Chamwino mkoani Dodoma, ambapo Rais Mstaafu Obasanjo ametoa salamu zake za rambirambi kwa Rais Samia Suluhu Hassan kufuatia vifo vya waliokuwa Marais wa Tanzania ambao ni Mzee Benjamin Mkapa na Dkt. John Magufuli.

Rais Mstaafu Obasanjo amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kupokea kijiti cha kuwa Rais wa Tanzania na amemtakia heri katika majukumu yake.

Aidha, katika mazungumzo hayo Viongozi hao wamezungumzia hali ya usalama Barani Afrika na umuhimu wa Wakuu wa nchi kujadiliana na kutafuta suluhisho la migogoro Barani humo inayosababisha vifo vya watu wasio na hatia hasa Wanawake na Watoto.

Pia Viongozi hao wamezungumzia masuala ya maendeleo hasa katika uchumi na kusisitiza umuhimu wa nchi za Afrika kuongeza ushirikiano na kuondoa vikwazo vya biashara na uwekezaji.