Na Mwandishi wetu

Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Tanzania (CDF) Jenerali Venance Mabeyo,ametembelea Ubalozi wa Jamhuriya Muungano wa Tanzania nchini Afrika Kusini.

Jenerali Mabeyo yupo Nchini Afrika Kusini kuhudhuria sherehe za kumuaga Mkuu Majeshi wa Afrika Kusini Jenerali SZ Shoki zilizofanyika kitaifa Jana Mjini Pretoria. Kuhudhuria sherehe hizi,ni utaratibu uliowekwa  na nchi wanachama wa Jumuiya za SADC ya maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) katika kuimarisha  mashirikiano  hususan katika nyanja ya Diplomasia ya Ulinzi (Defence Diplomacy) na Amani katika eneo Ia nchi za SADC.

Jenerali Mabeyo, alikaribishwa Ubalozini na Mhe. Balozi Mej. Jen. Gaudence Milanzi (Mst) na watumishi wa Ubalozi Mhe. Balozi Milanzi alitoa taarifa fupi ya eneo la uwakilishi ya Afrika Kusini, Botswana na Falme ya Lesotho.

Mhe. Balozi alieeza kuwa hali ya uwakilishi inaridhisha kiulinzi na kiusalama, Ubalozi umeendelea kukuza mashirikiano na nchiza eneo la uwakilishi ikiwa ni pamoja na SADC. Kwa kufuata miongozo ya sera ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inavyoelekeza kuendeleza Diplomasia ya kisiasa na kutekeleza Diplomasia ya uchumi.


Upande wake Jenerali Mabeyo alielezea ziara yake kwa ujumla nchini Afrika Kusini imekuwa ni ya mafanikio, na pia kuna mambo kama ambayo kama Mkuu  wa Majeshi ameona yanafaa kuigwa ili kuboresha utendaji wa Jeshi la Tanzania.

Jenerali Mabeyo amesema kuwa Rais wa Jamhuri ya  Muungano  wa  Tanzania Mhe. Samia Suluhu  Hassan, amelenga kuendeleza maendeleo ndani na nje ya nchi mfano katika kutekeleza Sera ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Muungano  wa Tanzania na mwelekeo  unaelekeza kuimarisha  Diplomasia kwa  kujenga mahusiano na nchi duniani kwa   kuimarisha Diplomasia ya siasa na Diplomasia ya uchumi.

Jenerali Mabeyo alimsihi Balozi na watumishi wa Ubalozi kuhakikisha kuwa wanaielewa na kuisimamia dira ya Diplomasia kama ilivyoainishwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan, ili kuweza kutelekeza majukumu yao kwa wepesi.