Na WAMJW- DOM.
Wataalamu wa Afya wa nchi 194 wamejadili namna ya kuboresha na kuimarisha mifumo ya ndani ya utoaji wa huduma za Afya ili kuzisaidia nchi wanachama kuwa tayari katika kukabiliana dhidi ya magonjwa mbali mbali ikiwemo magonjwa ya mlipuko.

Hayo yamejadiliwa katika Mkutano wa 74 wa Afya Duniani unaoendelea kupitia njia ya mtandao wenye lengo la kujadili mikakati mbali mbali na Sera za Afya ili kuboresha utoaji huduma za Afya kwa wananchi katika nchi wanachama wa Shirika la Afya Duniani (WHO).

Katika kikao hicho jumla ya nchi 194 zimeshiriki, ikiwemo nchi ya Tanzania na kutoa mikakati mbali mbali inayotekelezwa na nchi katika mapambano dhidi ya magonjwa mbali mbali ikiwemo ugonjwa wa Corona.

Kauli mbiu ya Mkutano huo ni “Komesha ugonjwa wa COVID-19 sasa, zuia ujao, ili kujenga pamoja Ulimwengu wenye afya na salama( Ending this Pandemic, Preventing the next, Building together a healthier, safer and fairer World).

Nchi wanachama, ikiwemo Tanzania zimeonesha mikakati mbali mbali iliyochukuliwa hasa katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Corona ikiwemo kuanzisha viwanda vya kutengeneza Barakoa (Mask), vipukusi (sanitizer) na nguo maalum za kujikinga watoa huduma wa Afya wakati wa kumuhudumia mgonjwa mwenye maambukizi ya Corona.

Mbali na hayo, nchi wanachama zimeshauriwa kuanzisha chombo cha kimataifa (International instrument) kitachoweza kusaidia kuweka mikakati mizuri katika kukabiliana dhidi ya magonjwa ya mlipuko na kutatua changamoto zitakazojitokeza hasa katika mlipuko wa ugonjwa wa Corona kwenye upatikanaji wa chanjo, vifaa vya kujikinga pamoja na teknolojia.

Aidha, Mkutano huo wa Wataalamu umependekeza nchi wanachama zitafakari faida ya kuwa na chombo hicho (International instrument) kitakacho rahisisha mapambano dhidi ya magonjwa mbali mbali ili kupeleka hoja hiyo kwa Mawaziri wa Afya wa nchi wanachama zote Duniani kujadiliwa na kupitishwa.

Mkutano wa Afya wa Dunia (Word Health Assembly) hufanyika kila mwaka nchini Geneva,kutokana na janga la Corona kwa miaka miwili Sasa unafanyika kwa njia ya mtandao.Mwaka huu mkutano huo umeanza kufanyika tarehe 24 Mei Hadi 1June, 2021.