Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro amewahakikishia Watanzania kuwa hali ya usalama nchini na nchi jirani ya Rwanda ni salama hii ni kutokana na makubaliano kati ya nchi hizo mbili kufuatia operesheni za pamoja katika kushughulikia uhalifu unaovuka mipaka, matishio ya ugaidi na matishio mengine ikiwemo usafirishaji wa binadamu na biashara za dawa za kulevya.

IGP Sirro amesema hayo leo jijini Dar es salaam, wakati alipokutana na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchi Rwanda, Kamishna Jenerali Dan Munyuza, ambaye yupo nchini kwa ziara ya kikazi ambapo Wakuu hao wamekubaliana kuendelea kushirikiana kwa pamoja na kubadilisha taarifa za wahalifu pamoja na kushughulikia uhalifu bila kuwa na vikwazo vya mipaka ili kuwahakikisha maendeleo ya kiuchumi  wananchi wa nchi zote mbili.

Kuhusu watu wanaoenda kujiunga na kundi la uhalifu nchini Msumbiji IGP Sirro amesema hadi sasa tayari Wakuu hao wa majeshi ya Polisi wamekubaliana kuweka mkakati utakaowezesha kuwapata wahusika ikiwa pamoja na kuwapata watu wanaofadhili makundi hayo yakihalifu ili sheria iweze kuchukua mkondo wake.

Kwa upande wake Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini Rwanda, Kamishna Jenerali Dan Munyuza amesema kuwa wamekubaliana kukutana mara kwa mara na kufanya mafunzo ya pamoja na kutekeleza makubaliana waliyoyafikia katika kukomesha matishio ya kigaidi pamoja na uhalifu mwingine ikiwemo uhalifu unaovuka mipaka.