Na. James K. Mwanamyoto-Mwanza
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Mohamed Mchengerwa ameitaka Idara ya Kumbukumbu na Nyaraka za Taifa kuboresha mifumo ya kidigitali ya kuhifadhi kumbukumbu na nyaraka muhimu za taifa ili kuimarisha usalama wa nyaraka hizo.

Mhe. Mchengerwa ameyasema hayo alipokuwa akizungumza na Watumishi wa Kituo cha Kumbukumbu Tuli Kanda ya Ziwa kilichopo Jijini Mwanza wakati wa ziara yake ya kikazi yenye lengo la kuhimiza uwajibikaji kwa Watumishi wa Umma.

Mhe. Mchengerwa amesema mifumo ya kidigitali ikiboreshwa, itapunguza uvujaji wa nyaraka na siri za Serikali, tatizo ambalo limekithiri kwa baadhi ya Watumishi wa Umma wasio waadilifu kutokana na ongezeko la matumizi ya mitandao ya kijamii.

“Siri nyingi za Serikali zimekuwa zikivuja sana, jambo ambalolimekuwa likileta aibu kwa taifa, hivyo ni lazima tuweke mifumo ya TEHAMA imara na madhubuti kudhibiti hali hiyo.” Mhe. Mchengerwa amesisitiza.

Aidha, Mhe. Mchengerwa ameitaka Idara hiyo kutoa elimu kwa umma kupitia vyombo vya habari ikiwemo mitandao ya kijamii ili wananchi waweze kujua umuhimu wa utunzaji wa kumbukumbu na nyaraka za taifa kwa mustakabali wa taifa letu.

Sanjari na utoaji elimu kwa umma, Mhe. Mchengerwa ameielekeza Idara hiyo kuwasisitiza Watumishi wa Umma nchini kutovujisha nyaraka za Serikali.

Akiwasilisha taarifa ya utekezaji wa Kituo cha Kumbukumbu Tuli, Kanda ya Ziwa, Kaimu Mkurugenzi, Bw. Firimin Msiangi amesema Kituo hicho kilianzishwa mwaka 1982 kwa lengo la kusimamia na kuratibu masuala ya utunzaji wa nyaraka katika eneo la Kanda za Ziwa.

Mhe. Mchengerwa yuko Mkoani Mwanza kwa ziara ya kikazi ya siku mbili ambapo atamalizia ziara yake Wilayani Magu kwa kuzungumza na Watumishi wa Umma na kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF.