Na Farida Ramadhani - WFP , Dodoma
Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) ameiagiza Mamlaka ya Usimamizi wa Bima nchini (TIRA) kutatua changamoto zinazoikabili sekta hiyo ili kuongeza wingo wa huduma za bima nchini.

Ametoa agizo hilo wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na uongozi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bima nchini (TIRA), walipokwenda kujitambulisha na kutoa taarifa ya utendaji wa taasisi hiyo ofisini kwake jijini Dodoma.

“Tunataka taasisi za Serikali zinazosimamia sekta mbalimbali za biashara na uwekezaji ikiwemo nyinyi TIRA kuwa wawezeshaji wa biashara hizo kuendelea kufanyika bila kikwazo”, alibainisha Mhe. Dkt. Nchemba.

Kwa upande wake, Kamishna wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bima nchini (TIRA), Dkt. Mussa Juma alimuahidi Mhe. Waziri kuwa taasisi hiyo itayafanyia kazi maagizo hayo kwa kuhakikisha changamoto zote zinapatiwa ufumbuzi ili kuimarisha sekta hiyo na kukuza uwekezaji.