NA. Angela Msimbira TAMISEMI
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Ummy Mwalimu ametoa maagizo kwa Menejimenti kuhakikisha wanaweka mikakati ya haraka ya kuhakikisha kuwa hakuna mtoto anayesoma akiwa chini ya mti.

Akiongea na Menejimenti leo wakati wa kuwapokea Katibu Mkuu Profesa Riziki Shemdoe na Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia Afya Dkt. Grace Magembe katika ofisi za Mtumba Jijini Dodoma Waziri Ummy amepiga marufuku watoto wa kitanzania kusome chini ya miti.

Akifafanua zaidi Waziri Ummy amesema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan ametoa maelekezo kuwa hataki kuona mtoto wa kitanzania akisoma chini ya mti , hivyo TAMISEMI ina wajibu wa kutekeleza maagizo hayo kwa kuhakikisha inaweka mikakati dhabiti ya jinsi ya kutatua kero hiyo.

“Mhe. Rais amesema hataki kuona mtoto wa Kitanzania akisoma chini ya mti au anakaa chini, watoto wote wasomee madarasani tena wakiwa wamekaa kwenye madawati” Amesma Mhe. Ummy.

Amewataka watendaji hao wakuu wa Wizara kuanza utekelezaji wa maagizo hayo ili kuondoa tatizo la hilo kabisa sambamba na kumaliza mlundikano wa wanafunzi mashuleni lengo likiwa kuboresha mazingira mazuri ya kujifunzia.

Kuhusu mlundikano wawanafunzi madarasani Waziri Ummy amesema kuwa inasikitika kuona baadhi ya shule nyingi nchini zinamlundikano mkubwa wa wanafunzi madarasani, hali hiyo ni hatarishi kwa wanafunzi na inapunguza uelewa wao.

“Napata tabu sana kuona watoto wanakaa mia mbili katika darasa moja na baadhi ya shule watoto wanabadilishana wengine wanakuja asubuhi na wengine mchana kutokana na uhaba wa vyumba vya madarasa , mimi siamini katika hilo kwa kuwa watoto wanaoingia mchana haweze kuwa makini katika kusoma lazima tubadilishe kwa kujenga vyumba vya madarasa vya kutosha” amesisitiza Waziri Ummy

Ameendelea kuweka wazi mikakati ya kuboresha Elimu kuwa ni pamoja na ujenzi wa maabara za kutosha na uwepo wa nyumba za walimu ili kuboresha mazingira ya kujifunza na kufundishia.

“Ni wakati sasa wa kutafuta rasilimali fedha kwa ajili ya kutatua changamoto hizo kwa kusimamia ukusanyaji wa mapato kwenye Halmashauri ili ziweze kazi hizi muhimu katika kukuza sekta ya Elimu Nchini.