Na Mwandishi Wetu
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Uratibu, Kazi,Vijana,Ajira na wenye Ulemavu, Jenista Mhagama ameagiza Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) kufanya tathmini ya maeneo ya kazi yanayoongoza kwa matukio ya ajali na magonjwa pamoja na kubainisha visababishi vyake ili kuwezesha uandaaji wa mkakati wa kudhibiti visababishi hivyo.

Ametoa agizo hilo alipokuwa akifungua kikao cha pili cha baraza la wafanyakazi wa OSHA kilichofanyika jijini Dodoma kwa lengo la kupitia bajeti ya mwaka 2021/2022.

“Taarifa iliyotolewa na Kaimu Mtendaji Mkuu inaonesha taasisi yenu imekuwa na mafanikio makubwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita ambayo yametokana na maboresho mbali mbali ambayo yamekuwa yakifanyika na serikali ikiwemo kuondoa baadhi ya tozo ambazo zilionekana kuwa kero.Hivyo, nawaagiza kuendelea kufanya kazi kwa weledi na uadilifu ili kuweza kufikia lengo letu la kupunguza ajali na magonjwa yatokanayo na kazi na kuleta ustawi wa Taifa letu,” alieleza Mhagama.

Waziri huyo wa Nchi aliwashauri wajumbe wa kikao hicho kufanya majadiliano katika kikao hicho kwa hekima na busara na hatimaye kutoka na maazimio muhimu ambayo yatafanyiwa kazi ili kutimizi malengo ya taasisi.

Aidha, aliitaka taasisi ya OSHA kuendelea kubuni mifumo mbali mbali ya Tehama ambayo itaboresha utoaji wa huduma kwa wadau pamoja na kuweka taratibu za huduma ambazo ni rafiki kwa wadau ili kuendana na maelekezo ya serikali.

Awali wakati akimkaribisha Waziri ambaye alikuwa Mgeni Rasmi katika kikao hicho, Kaimu Mtendaji Mkuu wa OSHA, Khadija Mwenda, amesema maboresho ambayo yamekuwa yakifanyika na serikali katika sekta ya biashara na uwekezaji ikiwemo kuondoa baadhi ya tozo, yamepelekea taasisi hiyo kupata mafanikio makubwa ikiwemo kuongeza usajili wa maeneo ya kazi kutoka 5,300 hadi 20,000 kwa kipindi kati ya mwaka wa fedha 2014/2015 na 2020/2021.

Kwa upande wao mwakilishi wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya (TUGHE) Taifa, Fidelis Athuman na Mjumbe wa Baraza hilo, Joyce Mwambungu, wameipongeza serikali na uongozi wa OSHA kwa maboresho ya utendaji ambayo yamekuwa yakifanyika kutokana na ushirikishwaji wa watumishi kupitia vikao vya mara kwa mara vya baraza la wafanyakazi.

Kikao hiki ambacho ni cha pili cha baraza la nne la wafanyakazi wa OSHA pamoja na masuala mengine, kilikuwa na agenda kuu ya kupitia bajeti ya mwaka  wa fedha ujao (2021/2022).

Mabaraza ya wafanyakazi katika taasisi mbali mbali za umma yapo kwa mujibu wa Sheria Na. 19 ya Mabaraza ya mwaka 2003 ambayo iliundwa kupitia Waraka wa Rais Na. 1 wa mwaka 1970. Lengo likiwa ni kuleta ushirikishwaji baina ya menejimenti na watumishi katika kufanya maamuzi yanayohusu utendaji wa taasisi husika.