Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega amewataka wananchi wa Kijiji cha Horohoro Kijijini Kata ya Duga katika Wilaya ya Mkinga mkoani Tanga, kutoruhusu mifugo ipitishwe kinyemela mpakani kwenda nchi jirani badala yake wawafichue wanaofanya hivyo ili kuwadhibiti kwani serikali inakosa mapato.

Ulega aliyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati alipofanya ziara ya kikazi wilayani humo kwa kutembelea eneo lenye ekari 23 ambapo kutajengwa mnada wa mifugo kijijini hapo na kusema kuwa mnada huo utakuwa chachu ya kuinua maendeleo ya wananchi na taifa kwa ujumla.

Alisema lazima wananchi wilayani hapo kuhakikisha wanakuwa mabalozi wazuri wa kudhibiti mifugo kupitishwa kinyemela kwenda nje ya nchi ili kuiwezesha serikali kukusanya mapato hatua ambayo itakuwa ni chachu kubwa kwao kuwezesha maendeleo.

“Niwaambie tu kwamba lazima hivi sasa tujipange kwa ujio wa fursa za mnada huu kwani baada ya miaka miwili eneo hili litakuwa na picha tofauti na ilivyokuwa hapo awali na litafungua ukurasa mpya wa maendelea kwenye eneo lenu na tumekubaliana wizarani jambo hilo litaanza mwezi wa tano, wazee wa duga mtupe ushirikiano kwa vijana wetu ambao watakuja kufanya kazi hapa.“ Alisema Ulega

“RC Shigella utakuwa umeacha alama kwa hili na nyinyi wananchi RC ametoa rai mnada huo usigeuke kuwa ni dude ambalo litakuwa limekaa halina shughuli za kufanya watu wanapitisha mifugo njia za panya na nyie mnawaona na hamtoi taarifa kuzuia jambo hilo.” Alifafanua


Naibu Waziri huyo alisema mnada huo ukianza kufanya kazi, eneo hilo litakuwa na shughuli mbalimbali ambazo zitawasaidia kuwaingizia vipato mbalimbali vya kimaendeleo hali ambayo itasaidia kuinua kipato cha mtu mmoja mmoja na
taifa kwa ujumla.

“Lakini niwaambie kwamba mkiacha watu wanapitisha mifugo kwa njia ya panya hakuna nchi inachokipata na wananchi hamuwezi kupata chochote hapo ni sehemu nzuri ya kuhakikisha mnapaombea na kupiga dua, sala tuweze kuinua uchumi wetu watu wa Mkinga.” Alisema

Aidha alisema mnada huo utaanza mwezi Mei mwaka huu, huku akiwataka wakazi wa eneo la Kata ya Duga kuwapa ushirikiano watumishi ambao watapelekwa kwa ajili ya kufanya kazi hiyo ya kuhakikisha wanakusanya ushuru wa serikali.

Aliwataka pia wafugaji wa eneo hilo kuhakikisha wanafuga kisasa ili waweze kuwa na ng’ombe wenye tija zaidi kutokana na kwamba watanzania wapo kwenye mazingira mazuri ya kufuga kisasa tofauti na nchi nyingine.

“Mhe. Rais wetu Samia Suluhu Hassan anataka kuona ng’ombe wenye kilo 500 diwani wa Kata ya Duga na wengine tunataka tukimbie mchakamchaka tufikie lengo la Rais anataka kuona tunauza nyama inatupa tija, mfugaji anabadilika anapata kipato na nchi inapata mapato ya kutosha.” Alisema

Naibu Waziri huyo alisema kuwa Mkuu wa Mkoa wa Tanga Martine Shigella alibainisha kuwa mkoa unataka kufanya mambo mbalimbali ya maendeleo lakini hayo yote hayawezi kufanikiwa ikiwa baadhi ya watu wanapitisha ng’ombe kwenda nje ya nchi kinyemela kwa kutumia njia zisizo rasmi.

Alifafanua kuwa ili kuongeza mapato ya serikali kupitia mifugo, katika mwaka ujao wa fedha 2021/2022 Wizara ya Mifugo na Uvuvi imepanga kutumia Shilingi Bilioni 4 na Milioni 400 kwa ajili ya kujenga minada mbalimbali nchini ukiwemo wa Kijiji cha Horohoro Kijijini kata ya Duga katika Wilaya ya Mkinga Mkoani Tanga.

Alisema ujenzi huo unatokana na takwa la kisheria la magonjwa ya wanyama namba 17 ya mwaka 2003 ambayo inataka kufanyika hayo huku akieleza kuwa wizara ina mipango mingi ya kuhakikisha wanawasaidia wafugaji kuhusu sehemu za malisho.

Awali akizungumza katika eneo hilo la mnada Mkuu wa Mkoa wa Tanga Martine Shigella alisema moja ya tatizo kubwa lililopo eneo la mpakani ni kutokuwa na mnada wa uhakika kwa ajili ya wafanyabiashara na wafugaji wa mifugo, ndiyo maana serikali ya Mkoa wa Tanga na Wizara ya Mifugo na Uvuvi zinataka kusiwe na ufugaji wa kuhamahama.

Shigella alisema hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan aliyoitoa bungeni hivi karibuni, ameeleza nia yake ya kutaka kuona wafugaji matajiri na siyo wa kuhamahama na ili kuweza kujenga mazingira wezeshi ya eneo la kuuzia mifugo kwani bila kufanya hivyo, wafanyabiashara wamekuwa wakienda kuwalangua wafugaji kwenye mazizi yao na hivyo kujikuta hawanufaiki ipasavyo.

“Kuna soko kubwa nchini Kenya ambapo baadhi ya wafugaji na wafanyabiashara wasiokuwa waaminifu walikuwa wanasafirisha mifugo kwenda Kenya na baadhi ya watumishi wa serikali wasiokuwa waaminifu ndio walikuwa wanaongoza mchakato huo wa kusafirisha mifugo bila kupitia kwenye taratibu mahususi zilizopo.” Alisema Shigella

Hata hivyo alisema anaishukuru wizara kwa kuliona hilo na kuunda kamati na kuweza kubaini uwepo wa changamoto walizokuwa wanalalamikia wafanyabiashara na wananchi wa Kijiji cha Horohoro Kijijini kwani kubwa walilokuwa nalo ni mifugo kupitishwa kwenye njia isiyokuwa rasmi, kutokana na kutokuwa na eneo maalumu ambalo mifugo kabla haijasafirishwa inatakiwa ipumzishwe mahali ambapo itakaguliwa magonjwa na kukusanywa kwa tozo kabla ya kusafirishwa kwenda nchi jirani.

Kwa upande wake Afisa Biashara wa Minada kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Basil Mataba alisema wizara ina jumla ya minada ya upili 14 na minada 11 ya mpakani ambapo mnada wa Kijiji cha Horohoro Kijijini mara utakapoanza kufanya kazi utakuwa wa 12.

Bw. Mataba alisema wanategemea Mwezi Mei mwaka huu mnada wa Kijiji cha Horohoro Kijijini utaanza kufanya kazi hivyo kuondoa adha ambazo walikuwa wakizipata wafanyabiashara na wafugaji kutorosha mifugo kwenda nje ya nchi ili kuuza mifugo yao.

Alibainisha hadi sasa eneo hilo la mnada tayari shughuli mbalimbali zinaendelea ikiwemo ya kufyeka nyasi na tayari kibanda cha kukusanyia ushuru kimeshasimikwa wakati wakiendelea na ujenzi wa eneo hilo huku akieleza kwamba wizara itaendelea na hatua za ununuzi wa vifaa kwa ajili ya uzio wa awali.