Rais Samia Suluhu Hassan amewaonya watumiaji wa mitandao ya kijamii wanaozusha uongo kuhusu chanzo cha kifo cha Hayati Dkt. John Magufuli aliyekuwa Rais wa tano wa Tanzania.

Amesema kuwa wapo wanaozusha kuwa Kiongozi huyo alipewa sumu, na kuwataka kama wana ushahidi wa kutosha wajitokeze wasikilizwe, vinginevyo waache kuleta uchonganishi ndani ya nchi.

Rais Suluhu Hassan ameeleza kuwa yanayosemwa na watu hao yanalenga kuchonganisha kabila na kabila, kundi moja la watu na jingine, na hatokubaliana na jambo hilo.

Alikuwa akilihutubia Bunge jijini Dodoma ikiwa ni mara yake ya kwanza tangu aapishwe kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Machi 19 mwaka huu kufuatia kifo cha Dkt. Magufuli.