Na Eliud Rwechungura
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Innocent Bashungwa ameagiza TCRA kuzifungulia TV za mtandaoni zote (Online TV) ambazo zilifungiwa ikiwa utekelezaji wa maelekezo ya Rais Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan aliyoyatoa April 06 ,2021 wakati akiwaapisha Makatibu wakuu, Manaibu Katibu Wakuu  na Wakurugenzi wa taasisi mbalimbali.

Waziri Bashungwa ametoa maelekezo hayo April 07, 2021 katika Makumbusho ya Taifa Dar es salaam alipokuwa akitoa ufafanuzi wa mambo mbalimbali kabla ya hafla uzinduzi wa filamu ya kumbukumbu ya kuenzi maisha na Kazi zilizofanywa na Hayari Dkt. John Pombe Magufuli, Aliyekuwa Rais wa awamu ya tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

''Kwa upendo wa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan ametuelekeza kwamba ili tuweze kuhakikisha tunalinda ajira zilizopo kwenye tasnia ya habari alitoa maelekezo kwamba TV zote za mitandao tuziruhusu ziweze kufanya kazi na ningependa kupitia kwenu waandishi wa habari niwajulishe watanzania kwamba maelekezo ya Rais wetu ya kuhakikisha Online Tv zote zifunguliwe, tayali tumeshalifanyia kazi. Mpaka sasa tuna TV za Mtandaoni (Online TV) 440 ambazo tumezisajili, kwa kushirikiana na Waziri mwenzangu wa Mawasiliano (Ndugulile) nimetoa maelekezo Online TV zote ambazo zilizuiwa zianze kufanya kazi lakini ni kwa kufuata masharti ya usajili na kuzingatia mashariti ya habari na utangazaji''

Waziri Bashungwa ameendelea kutoa ufafanuzi kwa upande wa magazeti ambapo ameeleza kuwa yalifungiwa kwa sheria huku akitoa wito kwa wamiliki kufika ofisni kwake ili kuangalia nini kilipelekea kufungiwa na nini kifanyike ili na wafunguliwe na kurudi katika utaratibu wa kutoa habari kwa mujibu sheria na utaratibu

“Kwa upande wa  haya magazeti ambayo  kwa sababu zotozote yalifungiwa, Sheria  ndizo zilitumiwa kuwafungia ndo maana nikasema  haya tutaenda nayo case by case, Ofisi yangu iko wazi, waje tuangalie nini kilipelekea kufungiwa na nini kifanyike ili warudi kwenye utaratibu wa kuendesha Vyombo vya Habari kwa mujibu wa sheria na kanuni za uendeshaji wa Vyombo vya Habari” ameeleza Bashungwa